RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewapa pole wafanyakazi waliokuwa na matarajio ya nyongeza ya mishahara na kuwaahidi kufanya hivyo Mei Mosi yam waka 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, tarehe 1 Mei 2021, katika Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza, kwenye maadhimisho ya kitaifa ya siku ya Mei Mosi.
Rais Samia amesema, ameshindwa kuongeza mishara kutokana na ugeni wake kwenye nafasi hiyo ya urais na kuahidi kutoa nafuu kwenye kodi katika bajeti ya mwaka 2021/22.
https://www.youtube.com/watch?v=vjbNTGs9Kso
Samia aliingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, baada ya kuapishwa kuchukua nafasi ya Hayati Rais John Pombe Magufuli, aliyefariki dunia tarehe 17 Machi 2021.
“Imekuwa ni vigumu kwangu na kwa sababu ndiyo nimeingia, sijakaa vizuri, kuongeza mishahara mwaka huu.”
“Kwa kutambua umuhimu wa wafanyakazi, tutaboresha maslahi kwa mwaka wa fedha 2021/22, kwa kupunguza viwango vya kodi ya mishara na mfumko wa bei lakini mwakani siku kama ya leo, nitapandisha mishahara ikiwemo kima cha chini. Nawapa pole kwa hili,” amesema Rais Samia Suluhu Hassan.
Rais Samia amesema, katika bajeti ya mwaka 2021/22, “tutapandisha vyeo watumishi 85,000 hadi 90,000, itatugharimu Sh.449 bilioni; Tutalipa malimbikizo ya watumishi Sh.60 bilioni; mabadiliko ya muundo Sh.120 bilioni na tutaajiri watumishi 40,000 Sh.239 bilioni. Kwa haya inakuwa ngumu kuongeza mishahara mwaka huu.”
Rais Samia, alikuwa akijibu maombi ya wafanyakazi waliyotolewa na Shirikisho la Wafanyakazi wa Tanzania (Tucta), la kuongezwa kwa mishara.
Tucta walisema, watumishi wa umma, hawajaongezewa mishahara kwa miaka sita huku wale wa binafsi wana miaka nane huku ugumu wa maisha ukiendelea na kupunguza molari ya kazi.
Leave a comment