RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amemfukuza kazi Mkuu wa Wilaya ya Maorogoro, Bakari Msulwa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro, Sheilla Lukuba, kwa kosa la kuruhusu matumizi ya nguvu, katika kuwaondoa wafanyabiashara wadogo ‘wamachinga’, katikati ya mji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza…(endelea).
Rais Samia ametangaza uamuzi huo leo Jumanne, tarehe 15 Juni 2021, akizungumza na vijana wa Tanzania, jijini Mwanza.
“Niliona juzi Morogoro vijana wajasiriamali wametengewa maeneo mbali na watu wanakofika, sababu hawauzi wamerudi eneo walilozoea. Nimeona mgambo wakiwavamiwa, kuwapiga na kuharibu vitu vyao,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Nimesikitika na hilo na niseme mkuu wa wilaya na mkurugenzi wa eneo lile hawana kazi. Sababu kuna njia nzuri zaidi ambayo wangeitumia na wale wakawaondosha kwa usalama. Si picha ile iliyojionesha kwenye TV.”
Tukio hilo lilitokea mwanzoni mwa Juni 2021, baada ya mgambo wa manispaa hiyo kuwavamia wamachinga waliorudi katikati ya mji na kuanza kuwapiga sambamba na kuharibu bidhaa zao.
Mgambo hao walikuwa wanatekeleza uamuzi wa Baraza la Madiwani la Manispaa ya Morogoro, wa kuwaondoa wamachinga katikati ya mji, kwa ajili ya kwenda kwenye soko maalumu lililotengwa na manispaa hiyo.
Leave a comment