WAZIRI wa Maji nchini Tanzania, Jumaa Aweso, ametengua uteuzi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira, Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, Mhandisi Robert Lupoja. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Aweso, amemteua Mhandisi Sadala Hamisi, kushika nafasi hiyo.
Taarifa iliyotolewa jana Jumatatu, tarehe 14 Juni 2021 na wizara hiyo imesema, Mhandisi Sadala kabla ya uteuzi huo, alikuwa mtumishi katika Wakala wa Majisafi na Mazingira Vijijini (RUWASA) DDCA.
Taarifa hiyo imesema, Awesso amefanya uteuzi huo kwa Mamlaka aliyopewa kwa mujibu wa sheria Na 5 ya mwaka 2019 ambapo Mhandisi Robert Lupoja atapangiwa majukumu mengine.
“Katika hatua nyingine Waziri wa Maji amevunja bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Sengerema na taratibu nyingine za Kiofisi zinaende kufanyiwa kazi” imeeleza, taarifa hiyo.
Aweso, alichukua uamuzi huo, saa chache kupita tangu Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kufanya ziara wilayani humo na kupokea kero mbalimbali ikiwemo ya maji.
Rais Samia, alionyesha kukerwa na kitendo cha mamlaka ya maji, kudaiwa fedha na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) akisema “sasa kama wananchi wanalipa bili ya maji, kwa nini fedha hizo hazitumiki kulipa Tanesco.”
Kutokana na hatua hiyo, Rais Samia alisema, kuna jambo la kufanya wialayani Sengerema kwani kuna mambo hayaendi sawa.
Leave a comment