RAIS Samia Suluhu Hassan amesema kuwa mafanikio ya kiuchumi yanayotokana na mbinu zinakiuka misingi ya haki na utawala bora hayawezi kuwa endelevu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Ameyasema hayo leo Alhamisi tarehe 24, Novemba, 2022,wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 27 wa Chama cha Wanasheria Afrika Mashariki.
Amesema hajawahi kuona Taifa lolote duniani ambalo limepata maendeleo ya kijamii na kiuchumi bila kuzingatia misingi hiyo.
“Sijawahi kuona Taifa ambalo limefikia mageuzi ya kweli ya kijamii na kiuchumi kwa kukiuka utawala bora na utawala wa kisheria, sijawahi. Na hata kama wakikua kiuchumi wanakua on papers lakini ukienda nje uchumi haukuwi kwa wananchi,” amesema Rais Samia na kuongeza;
“Hata kama taifa hilo lipo linaloendelea, huku juu kila kitu kizuri lakini watu ni wabovu nisingependa liwe ndani ya Afrika Mashariki yabakie mbali huko yasiwe kwetu.”
Amesisitiza kuwa kutenda haki na kuheshimu utawala bora ni misingi ambayo Serikali yeyote inayotokana na watu haina budi kufuata bila shinikizo lolote kutoka nje.
“Isipofata misingi hiyo hiyo Serikali sio ya watu na mnajua majina wanayoitwa,” amesema Rais Samia.
Amesema kutokana na hali hiyo Serikali ya sasa imeamua kuja na wazo la R nne ikiwa na maana ya “reconciliation, resilience, reform and rebuild of nation).
“Tumenza reconcilliation, vyama vya siasa tunazungumza tunaelewana, that is why mnasikia Tanzania imekaa vizuri na tutaendelea na jitihada hizo kusikiliza kila mtu wapi kuna gap, tukubali kukosoana na anayekosolewa akubali kujikosoa then turekebishe twende na matamanio yetu,” amesema
Amesema hayo si matamanio ya Serikali moja au nyingine, “ni matakwa ya msingi ya Katiba yetu Ibara ya 8 (1) yam waka 1977, inasema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi inayozingatia misingi ya kidemokrasia na haki ya jamii. Sasa ni tafsri ya anayekaa top kutafsi hii na kuendesha nchi.”
Amesema kwa upande mwingine ibara 6 ya Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inaeleza misingi ikiwepo utawala bora, kuzingatia misingi ya kidemokrasia utawala wa kisheria, uwajibikaji na uwazi.
“Tukikutana wenyewe anayekwenda kinyume tunamkalisha na kumsema kwahiyo kabla hujakalishwa na kusemwa tunajitahid kwenye nchi zetu kufuta misingi hiyo,” amesema.
Leave a comment