MBUNGE WA Sengerema (CCM), Hamis Tabasamu, amemshauri Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, afanye ziara katika nchi zinazozalisha mafuta, ili akaziombe ziuze nishati hiyo kwa gharama nafuu, kama alivyofanya Rais wa Awamu ya Kwanza, Hayati Mwalimu Julius Nyerere. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma….(endelea).
Tabasamu ametoa ushauri huo leo Ijumaa, tarehe 8 Aprili 2022, bungeni jijini Dodoma.
“Hali ilivyokuwa mbaya sasa hivi na kuelekea, tunamuomba Mama yetu Samia mahala ambako kuna hali ngumu asafiri mwenyewe kama Rais wa nchi, akazungumze na hawa wazalishaji wa mafuta, tuweze kupata mafuta kwa gharama nafuu,” amesema Tabasamu.
Mbunge huyo wa Sengerema amesema kuwa, miaka ya 1980 nchi ilipokabiliwa na changamoto ya uhaba wa mafuta kutokana na sababu za kiuchumi, Mwalimu Nyerere alifanya ziara katika nchi zinazozalisha mafuta ikiwemo, Lgeria, Saudi Arabia na Kuwait, kuomba mafuta na akafanikiwa.
Katika hatua nyingine, Tabasamu ameiomba Serikali ihakikishe Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), inalipwa fedha inazodai katika taasisi za umma, ikiwemo Shirika la Umeme la Tanzania, linalodaiwa Sh. 502 bilioni, ili liweze kuagiza mafuta nje ya nchi.
“TANESCO mpaka Januari 2022, anaidai bilioni 502, ukichukua Februari, Machi na Aprili atakuwa anaidai TANESCO bilioni 652, huyu TPDC ni kwamba anayo kampuni tanzu ya Tan Oil, ilikuwa imetengenezwa kusambaza mafuta kwa nchi,” amesema Tabasamu na kuongeza:
“Ushauri wangu kwa Serikali waje waeleze wanamlipa lini TPDC pesa ya kuagiza mafuta, mashirika kama haya yako duniani isipokuwa sisi Tanzania hili shirika limekuja kuonekana mfu halina kazi, kama tukiagiza mafuta yetu ikitokea shida tunasambaza.”
Loh!
Mbona hamsemi kuhusu magari ya umeme?
Hamjui Ulaya watasimamisha uzalishaji wa magari ya mafuta mwaka 2025?
Acheni kubweteka. Kazeni kamba zile V8 zipunguze safari.
“Omba omba mwisho utakula makombo”