RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi , amesema Serikali yake inakusudia kuboresha miundombinu ya bandari pamoja na hifadhi ya kutosha ya mafuta, ili kushusha bei yake inayotokana na kuhifadhiwa nje ya visiwa hivyo. Anaripoti Mwandishi Wetyu, Zanzibar … (endelea).
Rais Mwinyi ametoa taarifa hiyo leo tarehe 4 Machi 2023, akizindua Bohari ya Mafuta katika Bandari ya Mangapwani, visiwani Zanzibar.
Amesema uboreshwaji wa maeneo hayo utapelekea mafuta kusafirishwa moja kwa moja kutoka sokoni hadi Zanzibar, kitendo kitakachopunguza gharama za uhifadhi na usafirishaji.
“Kwa hali ya sasa Zanzibar hatuleti mafuta moja kwa moja, yakitoka Dar es Salaam yanahifadhiwa Tanga sababu hapa hatuna hifadhi ya kutosha, yakitoka Tanga yanaletwa Zanzibar. Haya yote yanasababisha mafuta kuwa na bei hii,” amesema Rais Mwinyi na kuongeza:
“ Nini tunataka kufanya, tukishakuwa na hifadhi ya kutosha na gati ya kutosha, meli moja kwa moja itashusha Zanzibar, tutakuwa na mafuta bei rahisi. Na huo ndiyo mpango na azma ya Serikali, tutafanya kila linalowezekana hilo litimie na maslahi ya nchi kwenda mbele.”
Leave a comment