RAIS wa Jamhuri ya Indonesia, Joko Widodo anatarajiwa kuwasili nchini leo Jumatatu kwa ziara ya siku mbili itakayoanza leo na kesho Jumanne tarehe 22 Agosti 2023. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ziara hiyo itakuwa ni ziara ya pili kwa kiongozi wa taifa hilo kutembelea Tanzania kwani ziara ya kwanza ilifanywa Rais wa Pili wa Indonesia, Soeharto tarehe 05 Disemba 1991, miaka 32 iliyopita.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na ushirikiano wa Afrika mashariki, Dk. Stergomena Tax amesema ziara hiyo ni matokeo ya kazi kubwa anayoifanya, Rais Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na mataifa mengine.
Amesema Rais Widodo atawasili tarehe 21 Agosti, 2023, na atapokelewa rasmi na Mwenyeji wake, Rais Samia tarehe 22 Agosti, 2023, Ikulu Dar es Salaam.
Amesema baada ya mapokezi, viongozi hawa watakuwa na mazungumzo ya faragha, na baadaye mazungumzo rasmi.
Ameongeza kuwa baada ya mazungumzo rasmi, kutakuwa na hafla ya utiaji saini hati za makubaliano ya ushirikiano kwenye sekta mbalimbali kama afya, nishati, madini, uchumi wa buluu, ushirikiano wa kimataifa, uhamaji na biashara na kuzungumza na waandishi wa habari.
“Baadaye Rais Widodo atashiriki dhifa ya chakula cha mchana iliyoandaliwa na Rais kwa heshima yake. Siku hiyo hiyo pia, Rais Widodo atatembelea Ofisi ya Ubalozi wa Indonesia uliopo hapa nchini kabla ya kuhitimisha ziara yake na kuondoka nchini,” amesema.
Amesema chimbuko la uhusiano kati ya Tanzania na Indonesia ni Mkutano wa Bandung uliofanyika mwaka 1955 ambapo nchi nyingi za Afrika na Asia zilikuwa katika utawala wa kikoloni kwa kipindi hicho.
“Kupitia Mkutano huo nchi hizo zilikubaliana kuimarisha ushirikiano ili kujikomboa kutoka katika utawala wa kikoloni, na ulikuwa ndiyo msingi wa kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi zisizofungamana na Upande Wowote (Non- Aligned Movement -NAM).
“Hivyo, Tanzania na Indonesia zina uhusiano wa muda mrefu na wa kihistoria. Uhusiano huo uliasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Rais wa Kwanza wa Indonesia Mheshimiwa Soekarno,” amesema.
Amesema uhusiano wa kidiplomasia ulianza mwaka 1964, ambapo Indonesia ilifungua Ubalozi wake nchini mwaka 1964 na kuwa miongoni mwa nchi za mwanzo kabisa kufungua Ubalozi wake nchini miaka michache baada ya uhuru. Aidha, Tanzania ilifungua Ubalozi wake nchini Indonesia Agosti, 2022, ambao niliuzindua.
Ameongeza kuwa mwaka 2024 Tanzania na Indonesia zitakuwa zinatimiza miaka 60 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kidiplomasia.
“Pamoja na kushirikiana katika harakati za ukombozi, tangu kuanzishwa ushirikiano wa kidiplomasia pamekuwepo na mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na; uwekezaji, na kilimo hasa ikizingatiwa Indonesia imepiga hatua kubwa katika kilimo cha zao za mchikichi kutokana na kuwa na mbegu bora ya zao hilo.
“Pamoja na teknolojia ya kisasa, ziara ya Rais Widodo nchini itapanua wigo wa ushirikiano katika zao la mchikichi utakaowawezesha wakulima wetu za zao hilo kunufaika na mbegu bora ya mchikichi, na hivyo kuwajengea uwezo na kuongeza uzalishaji wa mafuta ya kula,” amesema.
Leave a comment