MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, amesema mapambano ya kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi bado ni mfupa mgumu kwa Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumamosi, tarehe 27 Januari 2024, jijini Dar es Salaam, Prof. Lipumba, ugumu huo unatokana na baadhi ya mapendekezo ya wapinzani ambayo Serikali inayoongozwa na CCM imeyakataa hususan yale yaliyomo katika Rasimu ya Katiba ya Jaji Joseph Warioba.
“Pamoja na watu kupoteza maisha kudai Katiba Mpya na Tume Huru za Uchaguzi, Katiba yenye misingi ya demokrasia, tuweze kuwa na utawala bora unaoheshimu haki za binadamu, unaopambana na ufisadi na rushwa, bado mambo haya hatujaweza kufanikiwa,” amesema Prof. Lipumba.
Mwanasiasa huyo mkongwe nchini Tanzania, amesema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya hayati John Magufuli, iliweka kando mchakato wa upatikanaji katiba mpya ulioasisiwa na mtangulizi wake, Jakaya Kikwete, hivyo Rais Samia alivyoingia madarakani alionesha matumaini ya kuukamilisha lakini hadi sasa hakuna dalili ya ukamilishaji.
“Sasa alipofariki Dkt. Magufuli na Mama Samia kuwa Rais kufuatana na Katiba sisi tulikuwa na matumaini kwamba ana fursa za kuweza kukamilisha zile ahadi ambazo mwenzake Hayati Rais Magufuli alizitaja ndani ya Bunge kwamba anaweza akazikamilisha,” amesema Prof. Lipumba
Kauli hiyo ya Prof. Lipumba imekuja baada ya Rais Samia hivi karibuni kuweka msimamo wa serikali yake kuhusu mchakato wa upatikanaji wa katiba mpya, ambapo alisema utekelezaji wake utatanguliwa na utoaji elimu ya katiba kwa wananchi katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo.
Leave a comment