KIM Poulsen, kocha mpya wa Taifa Stars amelibakisha benchi lote la ufundi lilokuwa likitumiwa na Ettienne Ndayilagije wakiwemo makocha wasaidizi Selamani Matola na Juma Mgunda. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Benchi hilo la ufundi ambalo lilikuwa chini ya Ndayilagije, aliyeondoshwa baada ya matokeo mabovu ya timu hiyo katika michuano ya Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani (CHAN), iliyomalizika hivi karibuni nchini Cameroon.
Akiongea na waandishi wa habari leo, Poulsen amesema hakuona sababu ya kubadilisha benchi hilo ila kila mtu anapaswa kutimiza wajibu wake vizuri.
“Benchi la ufundi litabaki lilelile kama lilivyokuwa, nilikuwa na mazungumzo mazuri na Mgunda pamoja na Matola lakini pia nimeshakutana na Matola na tumeongea.
“Pamoja na kocha wa makipa na kocha wa viungo watabaki vilevile sikuona sababu ya mimi kuja hapa na kubadilisha kila kitu, ingawa akija kocha mpya anaangalia ni kivipi unafanya kazi yako, kikubwa kila mtu atimize majukumu yake vizuri kuanzia kwa wachezaji hadi benchi la ufundi,” alisema Poulsen.
Mgunda na Matola walianza kufanya kazi kama makocha wasaidizi chini ya Etienne Ndayilagije wakichukua mikoba ya Hemed Morroco aliyekuwa kocha msaidizi wakati wa Emmanuel Amunike na kuipeleka timu hiyo kwenye michuano ya kombe la mataifa Afrika AFCON.
Kwa sasa Matola ni kocha msaidizi wa klabu ya Simba, huku Mgunda akiwa kocha mkuu wa klabu ya Coastal Union iliyopo mkoni Tanga ilinayoshiliki Ligi Kuu Tanzania Bara.
Leave a comment