JESHI la Polisi mkoani Dodoma limewathibiti na kuwaua majambazi wanne wa kiume ambao majina yao bado hayajatambulika wenye umri kati ya miaka kati ya 25 na 30 waliokuwa katika harakati za kufanya tukio la unyang’anyi wa kutumia silaha.
Tukio hilo limetokea tarehe 25 Aprili 2023 muda wa saa tatu usiku Mtaa wa Mwangaza – Kisasa, Kata ya Dodoma Makulu,jijini Dodoma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yamelezwa jana tarehe 26 Aprili 2023 na Kamanda wa polisi Mkoa wa Dodoma, Martin Otyeno alipozungumza na waandishi wa habari juu ya tukio la wanaosadikiwa kuwa majambazi waliofanya jaribio la kuvamia nyumbani kwa Edina Kashashari (41) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Kisasa.
Kamanda Otyeno amesema majambazi hao walifanikiwa kuiba pesa taslim sh. milioni 1.1, simu ya Samsung moja na simu ndogo tatu baada ya watu hao kumtishia kumkata na mapanga ndipo mhanga alipiga kelele za kuomba msaada ambazo zilisikika kwa majirani na majirani hao kutoa taarifa kwa askari waliokuwa doria eneo hilo.
Ameleza kuwa askari hao walifanikiwa kufika kwa haraka na kuwakuta watu hao ambao walijihami kwa kutaka kuwashambulia askari kwa mapanga na askari hao kujibu mapigo kwa kuwafyatulia risasi ambazo ziliwajeruhi watuhumiwa hao maeneo mbalimbali ya miili yao.
Amesema majambazi hao walijificha nyuma ya ukuta wa fensi na kuruka ukuta huo na kwenda kumvizia Edina Kashashari wakati anatakaka kufunga mlango wa nyumba na kumtishia kumkata na mapanga kisha kumpora vitu hivyo.
Majambazi hao wanne walifariki dunia wakiwa wanapelekwa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kwa matibabu.
Leave a comment