BENKI ya NMB na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), kupitia Wakala wa Serikali Mtandao ‘eGovernment Zanzibar’ wamesaini makubaliano ya ushirikiano, yatakayowezesha mifumo ya benki hiyo kuingiliana na ile ya ZanMalipo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hatua hiyo itawezesha taasisi za SMZ kukusanya mapato kupitia matawi na mifumo ya kidijitali ya benki hiyo.
Hafla ya kusaini makubaliano hayo imefanyika Zanzibar leo Jumatano tarehe 16 Machi 2022.
NMB imesema imejipanga kuimarisha ushirikiano huo ambao utakuwa chachu ya ukuaji wa uchumi visiwani humo na inaamini utakuwa wa karibu zaidi, endelevu na wenye manufaa kwa SMZ na taasisi zake lakini pia utakaoleta maendeleo chanya.
Akizungumza kabla ya kusaini makubaliano hayo ya mwaka mmoja yenye kipengele kinachoruhusu mazungumzo na kuyarefusha, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, ameipongeza SMZ chini ya Rais Hussein Ali Mwinyi kwa mageuzi chanya ya kiuchumi yanayochakatwa na kusimamiwa na serikali yake kwa ustawi wa Taifa.
Ruth amesema makubaliano hayo ni chachu kwa taasisi yake kubuni suluhishi mbalimbali za Wazanzibar na Taifa ujumla na maendeleo ya kidijitali kwa ulimwengu wa sasa hayaepukiki, hivyo ushirikiano wao huo utakuwa na mchango chanya katika kuharakisha ukuzaji uchumi na kurahisisha utendaji wa Serikali.
“Makubaliano haya ni kielelezo tosha kuwa Serikali ya Zanzibar na NMB sasa tunaenda kushirikiana kuboresha huduma za ukusanyaji mapato na malipo, sambamba na kuwezesha mifumo yetu kuingiliana na ile ya ZanMalipo, hivyo kuwezesha Taasisi za SMZ kukusanya mapato kupitia matawi ya NMB na mifumo ya kidijitali ya benki yetu,” amesema Ruth.
“Kupitia makubaliano haya, NMB na eGovenment Zanzibar, tunaenda kutengenezea Kituo cha Pamoja cha Malipo Kidijitali ‘One Stop Center,’ cha Shirika la Bandari Zanzibar, ambacho kitampa mlipaji wa huduma mbalimbali ‘control number’ moja kwa ajili ya kufanyia malipo mbalimbili bandarini, badala ya namba tofauti tofauti.”
“Suluhisho hizi mbili zinazoambatana na makubaliano haya, zinaenda kuboresha utoaji huduma kwa wananchi, lakini pia kuongeza ufanisi katika ukusanyaji mapato na kuondoa kero ya muda mrefu wanaotumia wananchi kufanya huduma za malipo,” amesisitiza Ruth mbele ya wanahabari katika ukumbi wa Wizara ya Katiba na Sheria.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa eGovernment Zanzibar, Said Seif Said, ameishukuru NMB kwa kusaini makubaliano ya ushirikiano huo, ambao aliutaja kama muarobaini wa changamoto mbalimbali za kimalipo wanazokutana nazo wananchi wa Zanzibar, unaoenda pia kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato ya Serikali.
“Sisi eGovernment tunaamini ushirikiano huu ni chanya, utakaobeba tija kwa Serikali, hususani hiyo ‘One Stop Center’ ambayo itajikita katika kurahisisha mifumo ya malipo bandarini ambako tutatumia mifumo ya kidijitali kuongeza ufanisi kwenye makusanyo mbalimbali.
“Tunatarajia huu utakuwa ni mwanzo tu, tunategemea kufanya mengi makubwa kwa pamoja baina yetu na NMB. Bandarini ni sehemu ambako kumekuwa na changamoto za muda mrefu katika masuala mazima ya makusanyo, lakini kupitia makubaliano haya tunaamini yataondoa na kumaliza changamoto zote hizo,” amesema Seif.
Leave a comment