WABUNGE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamewakaribisha wabunge kutoka Chama cha ACT-Wazalendo na wale waliotimuliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kwa nderemo. Anaripoti Ragina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya Job Ndugai, Spika wa Bunge kutoa taarifa ya kuwakaribisha ambapo wale wa ACT-Wazalendo walitangulia na kufuatiwa 19 waliofukuzwa Chadema kwa madai ya usaliti.
Hii ni baada ya wale wa CCM walioteuliwa na Rais John Magufuli kutanguliwa. Wabunge hao ni Humphrey Polepole, Riziki Lulida, Dk. Dorothy Gwajima na Prof. Shukrani Manya.
Wakati wabunge hao 19 na wanne wa ACT-Wazalendo wakiingia ukumbini kwa makundi, walipigiwa meza na idadi kubwa ya wabunge wa CCM kuashiria kuwakaribisha.
Wabunge hao 19 wanaotajwa na Bunge kuwa ni wa Chadema ni Halima Mdee, Ester Bulaya, Esther Matiko, Nusrat Hanje, Grace Tendega.
Wengine ni Hawa Mwaifunga, Jesca Kishoa, Agnesta Lambat. Tunza Malapo. Ceciia Pareso, Asia Mwadin Mohamed, Felister Njau, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Stella Siyao, Salome Makamba, Anatropia Theonest na Conchesta Lwamlaza.
Wabunge wa ACT-Wazalendo ni Khatibu Saidi Haji (Konde), Salum Mohamed Shafi (Chonga), Omar Ali Omar (Wete) na Khalifa Mohamed Issa (Mtambwe).
Mdee na Bulaya wameingia bungeni wakiwa na mavazi meusi huku wakivaa barakoa kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19).
Pia wabunge hao wawili (Mdee na Bulaya), hawakuingia na wenzao hapo awali, walichelewa.
Leave a comment