SERIKALI kupitia Wakala wa Taifa wa hifadhi ya Chakula (NFRA) umeanza kugawa chakula cha bei nafuu kwa mikoa ambayo ina mfumuko mkubwa wa bei ya chakula.
Pia NFRA umeendelea kuimarisha hifadhi ya chakula nchini kwa kuongeza akiba ya chakula kutoka tani 58,000 hadi tani 110,000 kwa mwaka 2021/2022 huku ununuzi wa chakula kwa mwaka 2022/2023 ukiendelea. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa jijini hapa leo tarehe 22 Oktoba, 2022 na Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Milton Lupa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu majukumu ya NFRA na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka wa fedha 2022/23.
Amesema ununuzi wa nafaka kwa msimu wa huo unaendelea kupitia kanda za Sumbawanga, (mikoa ya Rukwa na Katavi), Songea (mkoa wa Ruvuma), Arusha (mkoa wa Manyara), Shinyanga (mkoa wa Kigoma), Makambako (mikoa ya Iringa na Njombe), Songwe (mikoa ya Songwe na Mbeya) na Dodoma.
Lupa amesema NFRA umejipanga kuhudumia maeneo mengine yatakayothibitika kuwa na mahitaji ya dharura na upungufu wa chakula huku akitoa wito kwa wananchi kujihifadhia chakula ili kuwa na akiba ya kutosha.
“Chakula hicho hutolewa kwa kuzingatia matokeo ya tathmini ya hali ya chakula nchini inayofanywa na serikali kupitia wizara ya kilimo kwa kushirikiana na wadau wengine,” amesema Lupa.
Aidha, amesema NFRA imekamilisha sehemu ya mradi na kuongeza uwezo wa kuhifadhi nafaka hadi tani 90,000 katika kanda za Arusha (Halmashauri ya Babati) na Sumbawanga na Mpanda.
Amesema utekelezaji wa mradi huo kwa ajili ya kuongeza uwezo wa kuhifadhi nafaka, ambapo ukikamilika utaongeza uwezo wa kuhifadhi kutoka tani 251,000 hadi tani 501,000.
“Kukamilika kwa mradi huo, kumeongeza uwezo wa kuhifadhi nafaka kutoka tani 251,000 hadi tani 341,000 na utekelezaji wa mradi katika maeneo mengine Dodoma, Songea, Shinyanga, Songwe na Makambako umefikia asilimia 85,” amesema.
Kuhusu suala la ajira amesema NFRA imetoa ajira za muda mfupi kwa wananchi zaidi ya 3,000 zinazochangia kipato kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.
“Ajira hizo zinatokana na kazi mbalimbali zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa zoezi la ununuzi wa nafaka, uhifadhi na kipindi cha uzungushaji wa nafaka na utekelezaji wa mradi wa kuongeza uwezo wa kuhifadhi nafaka,” ameeleza Lupa
Lupa amesema ili kukabiliana na makali ya mfumuko wa bei za nafaka Wakala kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo imeongeza upatikanaji wa nafaka katika masoko ili kuleta unafuu wa maisha kwa wananchi.
“Kwa kuanzia,Wakala unahudumia Halmashauri za Bunda, Sengerema, Geita, Nzega, Liwale, Nachingwea, Longido, Loliondo na Monduli ambapo takriban tani 3,000 zimepelekwa katika maeneo hayo,” amesema Lupa
Leave a comment