Benki ya NBC imetoa msaada wa vitanda 60 kwa ajili ya wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Tunamkumbuka iliyopo wilayani Bukoba mkoani Kagera ikiwa ni hatua ya benki hiyo kuunga mkono jitihada za shule hiyo kuwasaidia wanafunzi wa kike kuondokana na adha ya kutembea umbali mrefu baada ya kukamilisha ujenzi wa bweni la wasichana la shule hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu… (endelea)
Akizungumza kwenye hafla fupi ya uzinduzi wa bweni hilo uliokwenda sambamba na makabidhiano ya vitanda hivyo iliyofanyika shule
ni hapo mapema wiki hii, Mkurugenzi wa Wateja binafsi wa Benki ya NBC, Elibariki Masuke alisema vitanda hivyo vyenye thamani ya Sh milioni 14 vitatumika katika bweni hilo litakalokuwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 120.
“NBC tuliguswa na jitihada zilizoonyeshwa tayari na wadau mbalimbali wa katika kufanikisha ujenzi wa bweni hili wakiwemo wananchi wenyewe na serikali na hivyo kwa kutambua umuhimu wa elimu iliyo salama kwa mtoto wa kike tukaona ni vema tusaidie kufanikisha hili watoto wetu wasome katika mazingira salama zaidi,’’ alisema.
Kwa upande wake Katibu tawala wa mkoa wa Kagera, Profesa Faustine Kamuzora pamoja na kuishukuru benki hiyo kwa msaada huo pia aliiomba kuweka msukumo katika ufundishaji wa somo la fedha na matumizi yake katika shule za sekondari ili kuwajengea msingi wa nidhamu ya fedha tangu wakiwa wadogo.
“Kwa kuwa mitaala yetu haizungumzii sana masuala ya elimu ya fedha kwa wanafunzi ni vema taasisi za kifedha zinazoguswa na masuala ya elimu kama ilivyo benki ya NBC kuangalia namna ya kusaidia katika kutoa mafunzo kwa wanafunzi wakiwa wadogo ili waweze kuanza kuelewa nidhamu ya fedha na matumizi yake wakiwa wadogo,’’ alisema.
Naye Mkuu wa Shule hiyo, Robert Muganyizi alisema ujenzi wa bweni hilo uliombatana na msaada wa vitanda vilivyotolewa na benki ya NBC utasaidia sana wanafunzi hao ambao hapo awali walikuwa hawapati muda wa kujisomea kutokana na uchovu waliokuwa wanaupata kwa kutokana na wao kutumia muda mwingi kutembea kurudi na kwenda hapo huku wakihatarisha usalama wao nyakati za usiku.
“Kuzinduliwa kwa bweni hili kutawaweka katika mazingira bora kitaaluma tofauti na ilivyokuwa mwanzo ambapo walikuwa wakilazimika kutembea zaidi ya kilometa thelathini na mbili ili kufika shuleni wakiwa wamechoka na hivyo kuzorotesha hata jitihada zao kimasomo. Tunashukuru sana wadau wote waliojitokeza kufanikisha hili ikiwemo benki ya NBC kwa msaada wao wa vitanda,’’ alisema.
Aidha, Ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kike katika shule ya sekondari Tunamkumbuka umegharimu zaidi ya shilingi milioni 63 ambapo NBC imechangia shilingi milioni kumi na nne, Mfuko wa Maendeleo Tanzania TDT ukichangia shilingi milioni 32 huku jamii ikichangia zaidi ya shilingi milioni 16.
Leave a comment