OFISI ya Sheikh Ahmed Dalmook Al Maktoum, Mwanafamilia ya Kifalme ya Dubai kutoka Falme za Kiarabu, imesaini mkataba wa makubaliano (MOU) na Serikali ya Tanzania, kupitia Wizara ya Kilimo, ili kutekeleza mpango wa usambazaji wa kimkakati na uhifadhi wa mbolea nchini kwa usalama wa chakula. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Makubaliano hayo pia yamelenga kusambaza mbolea ya uhakika na yenye ubora nchini ili kusaidia sekta ya kilimo kukua na kuboresha usalama wa chakula.
Chini ya masharti ya makubaliano hayo, Ofisi binafsi ya mwanamfalme huyo pamoja na washirika wake itaendeleza na kuendesha kituo cha kisasa cha kuhifadhi mbolea nchini Tanzania, ambacho kitakuwa na uwezo wa kuhimili usambazaji wa kimkakati wa bidhaa za mbolea.
Serikali ya Tanzania pia itawezesha katika kutoa miundombinu iliyopo katika maeneo tarajiwa. Kituo hicho kitawekwa kimkakati ili kuhakikisha kuwa wakulima kote nchini wanapata mahitaji ya mbolea kwa bei shindani.
Serikali ya Tanzania imekubali kupunguza kiasi cha mbolea kwa ajili ya kusambazwa kwa wakulima kote nchini. Ushirikiano huu utasaidia kuhakikisha wakulima wa Tanzania wanapata mbolea ya hali ya juu ambayo ni muhimu kwa ukuaji wa mazao na mafanikio ya sekta ya kilimo kwa ujumla.
Akizungumza baada ya kusaini mkataba huo, Sheikh Ahmed Dalmook Al Maktoum alisema “Tuna furaha kubwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kusaidia sekta ya kilimo, Makubaliano haya yanawakilisha hatua kubwa ya maendeleo katika juhudi zetu za kuwapatia wakulima nchini Tanzania mbolea ya hali ya juu wanayohitaji ili kukuza mazao yenye afya na kuboresha maisha yao.”
Ushirikiano huo wa kimkakati utasaidia kukuza ukuaji wa uchumi, kuboresha usalama wa chakula, na kuendeleza kilimo endelevu nchini.
Ofisi binafsi ya mwanamfalme huyo imedhamiria kufanya kazi kwa karibu na Serikali ya Tanzania ili kuhakikisha mpango huu unafanikiwa na inatarajia ushirikiano wa muda mrefu na wenye tija.
Ofisi binafsi ya Sheikh Ahmed Dalmook Al Maktoum inajishughulisha na miradi ya kilimo, nishati, miundombinu, madini, biashara ya bidhaa za mafuta na gesi, pamoja na elimu.
Leave a comment