OFISI ya Msajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, imekiandikia barua Chama Kikuu cha Upinzani nchini humo, Chadema, ikikitaka kijieleze juu ya kauli iliyotolewa na Katibu Mkuu wake, John Mnyika dhidi ya Rais Samia Suluhu Hassan. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana Alhamisi, tarehe 12 Agosti 2021 na Mnyika, katika ukurasa wake wa Twitter.
Kupitia mtandao huo, Mnyika amesema ofisi hiyo inakituhumu Chadema kwa kosa la kutumia lugha chafu dhidi ya Rais Samia.
Kauli hiyo chafu inadaiwa kutolewa na Mnyika, wakati akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam, tarehe 10 Agosti 2021, ambapo alidai Rais Samia alitoa kauli za uongo katika mahojiano yake na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC).
“Msajili wa Vyama ameniletea barua tarehe 12 Agosti 2021, kutaka niwasilishe maelezo tarehe 13 Agosti 2021 kwa kusema kuwa Rais alitoa kauli za uongo kwenye mahojiano yake na @bbcswahili . Amedai kutumia maneno hayo ni lugha chafu, kashfa na kinyume na maadili,” imesema taarifa ya Mnyika.
MwanaHALISI Online imemtafuta kwa simu Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Sixty Nyahoza, kuhusu suala hilo, ambaye amejibu “Ndiyo tumeandika barua na tumewaisilisha.”
Leave a comment