BUNGE la Tanzania limetanganza mchakato wa kujanza nafasi ya naibu spika wa Bunge ambapo uchaguzi wake utafanyika tarehe 11 Februari 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Uchaguzi huo unafanyika kujaza nafasi hiyo iliyoachwa wazi na Dk. Tulia Ackson ambaye alijiuzulu tarehe 31 Januari 2022, baada ya kuteuliwa na chama chake- Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwania uspika.
Dk. Tulia alikuwa miongoni mwa wagombea tisa waliojitokeza kugombea uspika Jumanne iliyopita ya tarehe 1 Februari 2022 na kushinda kwa kura zote za wabunge 376 waliopiga kura sawa na asilimia 100.
Dk. Tulia amechukua nafasi ya Job Ndugai ambaye tarehe 6 Januari 2022 alitangaza kujiuzulu.
Ndugai alichukua uamuzi huo baada ya kushinikizwa na viongozi wa CCM kutokana na kauli yake ya kukosoa mwenendo wa serikali kukoka fedha nje za kugharamikia miradi ya maendeleo kokosolewa vikali.
Leo Alhamisi, tarehe 3 Februari 2022, Ofisi ya Bunge imetoa taarifa kwa umma kikivitaarifu vyama vyenye uwakilishi bungeni kuweza kuanza mchakato wa kujaza nafasi hiyo.
“Chama kinachokusudia kushiriki uchaguzi, kinashauriwa kuanza mchakato wa kumpata mgombea kutoka miongoni mwa wabunge wa chama hicho,” imeeleza taaifa hiyo na kuongeza:
“Uchaguzi umepangwa kufanyika tarehe 11 Februari 2022. Hivyo jina la mgombea linapaswa kuwasilishwa kwa msimamizi wa uchaguzi kabla ya saa 10:00 jioni ya tarehe 10 Februari 2022, katika ofisi ya katibu wa Bunge.”
Leave a comment