RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa pole kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla na wafanyabiashara wa Soko Kuu la Kariakoo, kufuatia hasara kubwa waliyoipata kutokana na kuungua moto kwa soko hilo lililopo jijini humo. Anaripoti Ibrahim Yamola, Dar es Salaam … (endelea).
Moto ulioibuka jana usiku Jumamosi, umeteketeza soko hilo upande wa juu huku chini (shimoni) kukiwa hakujaathirika na moto huo ambao tayari vikosi vya ulinzi na usalama, vimekwisha kuuzima.
Leo Jumapili, tarehe 11 Julai 2021, taarifa iliyotolewa na Jaffar Haniu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, imeeleza kuwa, Rais Samia ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kufanya uchunguzi wa kina kujua chanzo cha moto huo.
Soma zaidi:-
Majaliwa akagua moto soko la Kariakoo, atoa siku saba
Rais Samia, amesema Soko Kuu la Kariakoo ni soko kubwa jijini Dar es salaam ambalo lina mkusanyiko mkubwa wa wafanyabiashara na kuteketea kwa soko hilo kutakuwa kumesababisha hasara kubwa kwa wapangaji na wamiliki wa soko hilo kongwe nchini.
Amesema Soko la Kariakoo licha ya kuajiri wafanyabiashara wengi lakini ni kitovu cha biashara kwa nchi za Afrika Mashariki hivyo tukio hilo si hasara kwa wafanyabiashara tu bali hata kwa Serikali.
Mapema leo asubuhi Jumapili, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ametembelea soko hilo na kutoa siku saba kwa za awali kamati aliyoiunda kuchunguza chanzo cha moto katika soko hilo ili kubaini nini kimesababisha au nani kasababisha moto huo.
Kamati iliyoundwa ambayo itafanya kazi na kamati ya ulinzi na usalama iliyoanza kufanya kazi chini ya Mkuu wa Mkoa huo itajumuisha Ofisi ya Rais-Ikulu, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo itawakilishwa na Mkurugenzi wa Maafa.
Wengine ni Vyombo vya Ulinzi na Usalama ikujumuisha Jeshi la Wananchi, Jeshi la Polisi, Zimamoto pamoja na Taasisi ya Kupambana na Rushwa.
Pia, Waziri Mkuu alizitaja Wakala wa Majengo, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).
Leave a comment