KATIBU Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) nchini Tanzania, John Mnyika amesema, mgombea wao wa urais atakwenda kuchukua fomu za urais Ofisi za Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) tarehe 8 Agosti 2020 saa 5 asubuhi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mnyika ametoa kauli hiyo leo Jumanne tarehe 4 Agosti 2020 katika mkutano mkuu wa Chadema unaofanyika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Mkutano mkuu huo utakuwa na ajenga mbalimbali ikiwemo kumthibitisha Tundu Lissu kuwa mgombea urais wa chama hicho na Salum Mwalimu, mgombea mwenza.
Pia, Said Issa Mohamed, atathibitishwa kuwa mgombea urais wa chama hicho upande wa Zanzibar.
Akizungumza kabla ya kuanza kwa mkutano huo, Mnyika amesema, amekwisha kumwandikia barua mkurugenzi wa NEC kumjulisha tarehe ambayo mgombea wao atakwenda kuchukua fomu.
Soma zaidi:-
“Uchaguzi wa Serikali za mitaa, walifanya hujuma nyingi za kinyume cha sheria ili wapite bila kupingwa na imekuwa ikifanyika hivyo mara kadhaa,” amesema Mnyika.
“Hatua hiyo ya kuhujumu wagombea, imekuwa ikifanyika hasa hatua ya kuchukua fomu na kurejea fomu lakini sasa basi. Kwa sababu sasa basi ni muhimu nguvu ya umma, ianze kuonekana hatua ya kuchukua fomu ili mambo yote yachukue,” amesema Mnyika huku akishangiliwa
“Tarehe 8 Agosti 2020 saa 5 asubuhi, mgombea wetu atakwenda kuchukua fomu Dodoma,” amesema Mnyika.
Katibu mkuu huyo pia amesema, tarehe 12 Agosti 2020 siku ya kwanza ya uchukuaji na urejeshaji fomu za udiwani na ubunge amesema, wagombea wote wa nafasi hizo wajitokeze kwa wingi kwenda kuchukua fomu ili kuepuka hila zinazoweza kujitokeza.
Mkutano huo umehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kisiasa, dini na asasi za kiraia.
Baadhi yao ni Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Maali Seif Sharif Hamad, Msajili msaidizi wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahonza na Msemaji wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Rajabu Katimba.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali ya kinachoendelea
Leave a comment