KATIKA mwaka wa fedha 2021/2022 Wakala ya Barabara (TANROADS), Mkoa wa Pwani unatarajia kutumia Sh. milioni 700 kwa ajili ya karabati wa barabara ya Bagamoyo hadi Msata. Anaripoti Selemani Msuya, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yamesemwa na Meneja wa TANROADS Pwani, Mhandisi Andrea Kasamwa wakati akizungumza na waandishi wa habari jana wilayani Bagamoyo ambapo Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB) ilikuwa inakagua miundombinu mbalimbali mkoani humo.
Mhandisi Kasamwa alisema TANROADS mkoa wa Pwani wamekuwa wakifanyia matengenezo barabara na mifereji jambo ambalo linachangia kudumu kwa muda mrefu.
“Mwaka wa fedha 2021/2022 tunatarajia kutumia Sh. milioni 700 kufanya matengenezo ya barabara, madaraja na mifereji kwenye barabara kutoka Bagamoyo hadi Msata ili kuhakikisha inadumu kwa muda mrefu,” alisema.
Meneja huyo alisema katika kutunza barabara za mkoa huo wamekuwa wakishirikisha wananchi jambo ambalo linasaidia kupata taarifa kwa wakati inapotekea uharibifu.
Alisema pia wanaendelea kufanya matengenezo ya barabara nyingine pale ambapo wanapata fedha lengo likiwa ni kuhakikisha barabara za mkoa huo zinazosimamiwa na TANROADS zinapitika muda wote.
Aidha, Kasamwa alisema TANROADS Pwani watatekeleza maelekezo na maagizo ambayo yametolewa na RFB kuhusu kukarabati miundombinu.
Meneja wa RFB, Eliud Nyauhenga alisema ili miundombinu ya barabara iweze kudumu ni jukumu la mameneja wa barabara kutumia fedha wanazopatiwa kwa umakini na uangalifu.
Alisema Serikali ipo tayari kutoa fedha ili kufanyia matengenezo ya madaraja, barabara na mifereji lakini haitamvumilia meneja ambaye atatumia fedha hizo kinyume na taratibu.
“Mfuko utatafuta fedha na kuzigawanya katika mikoa yote, kinachotakiwa ni fedha hizo zitumike kwa kazi ambayo imepangwa, tukigundua matumizi yana shida hatumvumilia mtu,” alisema.
Alisema Serikali imejipanga kumaliza changamoto ya miundombinu ya barabara, madaraja, na miferejeji hivyo lengo hilo litafanikiwa iwapo wanaosimamia mchakato huo watatumia fedha hizo kwa matumizi sahihi.
Aidha, meneja ametoa rai kwa Watanzania hasa wanaoishi karibu na barabara kuwa walinzi wa miundombinu hiyo kwa kuwa ni muhimu kwa shughuli za uzalishaji, usafiri na nyinginezo.
Leave a comment