HATIMA ya wabunge wanne wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kuendelea kusota lupango au kuwa nje kwa dhamana, wakati wakiendelea kusubiria kesi yao inayowakabili, yaweza kujulikana rasmi kesho, Jumatano. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Wabunge wanaosubiri maamuzi ya mahakama kujua hatima yao ya dhamana, ni Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini), Halima Mdee (Kawe), John Heche (Tarime Vijijini) na Ester Bulaya (Bunda Mjini).
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, iliamuru kukamatwa kwa wabunge hao, Ijumaa iliyopita, kufuatia kushindwa kufika mahakamani.
Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Thomas Simba alieleza kuwa amefikia maamuzi ya kutoa amri ya kuwakamata Heche, Msigwa, Mdee na Bulaya, baada ya kujiridhisha kuwa wameshindwa kufika mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili na bila mahakama kuelezwa walikokuwa.
Mdee alikamatwa nyumbani kwake Kawe, usiku wa Jumamosi iliyopita; huku Msigwa na Heche, wakikamatwa jana Jumatatu, walipokwenda kwenye Mahakama ya Kisutu kujisalimisha. Bulaya alijisalimisha leo asubuhi.
Wote wanne, wamekabidhiwa kwa jeshi la Polisi kwa ajili ya kuhifadhiwa mpaka kesho, mahakama itakapotoa maamuzi yake.
Leave a comment