IMETAJWA kuwa migogoro ndani ya ndoa au kwenye familia zilizo nyingi imechangia kwa kiasi kikubwa cha kuwepo kwa kazi kubwa ya watoto wa mitaani na waishio katika mazingira magumu. Anaripoti Danson Kaijage, Kondoa … (endelea).
Hayo yameelezwa hivi karibuni na Mwenyekiti wa Friends Of Mc Mwangata Assosiation (FOMMA) Dk. Gasper Kisenga mapema muda mfupi baada ya kukabidhi misaada mbalimbali ya kibinadamu kwa nyumba ya kulelea watoto yatima ijulikanayo kama Poloni Orphant’s House iliyopo wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma ambayo ipo chini ya kanisa Katholiki.
Akizungumza na watoto yatima wa kituo hicho pamoja na walezi wa watoto hao pamoja na wanaumoja wa FOMMA Dk. Kisenga alisema kuwa migogoro ndani ya familia imepelekea kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa ongezeko la watoto wa mitaani pamoja na watoto yatima ambapo wakati mwingine vifo vinatokea kwa sababu ya wanafamilia husika kufikia hatua ya kuuana.
“Tunajua kuwa yapo mambo mengi ambayo yanaweza kusababisha mtoto kuwa yatima au kuishi katika mazingira magumu lakini kwa sasa tumekuwa tukishuhudia vitendo vya kikatili ambavyo vinafanywa na wana familia ikiwa ni kuuwana, mama kumtelekeza mtoto au baba wa familia kutelekeza familia na kusababisha watoto wadogo kuingia mitaani kwa ajili ya kutafuta riziki.
“Pia vitendo vya kikatili navyo vinachangia kwa kiasi kikubwa cha kuwepo kwa wafamilia kujikuta katika mazingira magumu ambapo wakati mwingine kunasababisha kuwepo kwa mmomonyoko wa maadili jambo ambalo linasababisha watoto wengi kujikuta wanaharibikiwa au wanajiingiza katika mazingira ambayo hayafai” alieleza Dk.Kisenga.
Kutokana na hali hiyo Mwenyekiti huyo alisema kuwa umoja huo wa FOMMA umekuwa ukitoa misaada mbalimbali ya kibinadamu kwa vituo vya kulelea watoto yatima na wasiojiweza na kwa sasa wameweza kutoa misaada katika vituo mbalimbali katika jiji la Dodoma, Wilaya ya Chamwino na Wilaya ya Kondoa huku akieleza kuwa umoja huo unajipanga zaidi kuifikia mikoa nyingize yenye watu wenye uhitaji.
Hata hivyo alieleza kuwa misaada hiyo ni misaada inayotolewa na wana umoja huo kwa kuchangishana kama sadaka na kueleza kwamba hakuna ufadhiri kutoka nje ya nchi ,huku akiwaonya baadhi ya watu ambao wanatumia kivuli cha kutunza watoto yatina ma wenye uhitaji kwa maslahi yao binafsi.
Naye mwanzilishi wa FOMMA John Mwangata maarufu kwa jina la Mc Mwangata kakikabidhi msaada huo kwa watoto wa kituo hicho alisema kuwa lengo la umoja huo ni kuwafikia watoto wenye uhitaji ili nao wafarijike na kujiona ni sehemu ya watoto wanaoishi mazingira ya kawaida.
“Tunafanya hivi kwa ajiri ya kuonesha upendo kwa watoto ambao ni taifa la baadaye na viongozi wa baadaye na tunachangishana kama sehemu ya sadaka, tunajua wapo watu ambao wanatunza watoto lakini changamoto kubwa ni jinsi ya kuweza kuwatunza kwa kuwapatia huduma zote za kibinadamu.
“Mimi kama Mc Mwangata siwezi kuwafikia watoto waliowengi lakini kupitia umoja wetu tumeweza kuwafikia watoto wengi kwa kuwapatia misaada mbalimbali na leo tumewapatia watoto wa kituo hiki cha koloni Kondoa, sukari, mchele, mafuta ya kupikia, sabuni ya kufulia na kuogea, mafuta pamoja na zawadi mbalimbali ambazo ni viburudisho kama vile biskuti na jiusi” alieleza Mwangata.
Kwa upande wake Mlezi msaidizi wa nyumba hiyo , Sister Monica Irine akitoa shukrani zake kwa FOMMA baada ya kupokea misaada hiyo alisema kuwa kituo hicho ambacho cha kulea watoto yatima kinapokea watoto kuanzia siku moja hadi miezi sita ambao wamefiwa na wazazi wao wote au kupoteza mzazi mmoja na familia haiwezi kumtunza.
Alieleza kuwa nyumba hiyo ambayo ilianzishwa mwaka 1947 imekuwa ikipokea watoto kutoka Mikoa mbalimbali ya Tanzania kwa kufuata utaratibu wa kiserikali na pale mtoto apotimiza miaka sita kwa umri wa kutoka kituoni hapo umtoa kwa utaratibu wa kiserikali kwa kushirikiana na ustawi wa jamii.
Hata hivyo alisema kuwa bado kuna changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na ndugu wa watoto kutofika nyumba hiyo kabisa kwa ajili ya kujua maendeleo ya watoto wao na wakati mwingine kushindwa kuwachukua pale ambapo wanakuwa wamisha fikisha umri wa kutoka kituoni hapo.
“Wazazi wengine au ndugu wa watoto wanawatelekeza watoto kabisa hapa kituoni watoto wakisha fikishwa kituoni baadhi ya ndugu wa watoto hawaji kituoni wala kuwajulia hali na kukata mawasiliano kabisa na inapofikia umri wa watoto kutoka kituoni ndugu hwajitokezi jambo ambalo linawazimisha wasimamizi wa kituo hicho kuendelea kuwalea na kulazimika kuwapatia elimu jambo hilo ni changamoto kubwa kwetu” alieleza Sister Monica.
Aidha ameziomba taasisi mbalimbali na mtu binafsi kuiga mfano wa FOMMA kwa kuonesha upendo kwa watoto waishio katka mazingira magumu pamoja na yatima kwa maelezo kuwa kituo cha kulelea watoto hao kinakabiliana na changamoto nyingi ikiwemo gharama kubwa za uendeshaji kwa maana ya gharama za kuwatunza watoto hususani wale wachanga.
Leave a comment