WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema katika kipindi cha Julai 2021 hadi Aprili 2022, mfumuko wa bei umeongezeka hadi kufikia asilimia 3.9 kutoka asilimia 3.3 iliyokuwa kwenye kipindi kama hicho 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Dk. Mwigulu ametoa taarifa hiyo leo Jumanne, tarehe 7 Juni 2022, bungeni jijini Dodoma, akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha wa 2022/23.
“Mfumuko wa bei ulifikia wastani wa asilimia 3.7 kwa 2021 ikilinganishwa na asilimia 3.3 kwa 2020. Aidha, kipindi kama hicho Julai 2021 hadi Aprili 2022, mfumuko wa bei ulikuwa wastani wa asilimia 3.9 ikilinganishwa na asilimia 3.3 katika kipindi kama hicho 2021,” amesema Dk. Mwigulu.
Dk. Mwigulu amesema, ongezeko hilo limesababishwa na ongezeko la gharama za uzalishaji na usambazaji wa bidhaa na huduma hususan bidhaa za petrol, mafuta ya kula, mbolea na malighafi za viwandani.
“Pamoja na ongezeko hilo, kiwango hicho bado kipo ndani ya matarajio ya wigo wa nchi za Afrika Mashariki ambacho ni asilimia 3.0 hadi asilimia 5.0 na lengo la nchi za SADC asilimia 8.0,” amesema Dk. Mwigulu.
Katika hatua nyingine, Dk. Mwigulu amesema hadi kufikia Aprili 2022, wastani wa fedha taslimu uliongezeka kwa asilimia 13.8 ikilinganishwa na asilimia 2.7, katika kipindi kama hicho 2021.
Huku ujazo wa fedha ulikuwa wastani wa asilimia 13.1, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 6.8 kipindi kama hicho kwa 2021.
“Ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi uliongezeka na kufikia kwa 8.4, ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 4.3 kwa mwaka 2021.
Aidha, akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Marekani bilioni 4.56, kiasi ambacho kinatosheleza uagizaji bidhaa na huduma kutoka nje kwa kipindi cha miezi 4.8, ikilinganishwa na lengo la asilimia 4.0,” amesema Dk. Mwigulu.
Leave a comment