Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, imeishauri Serikali kuiongezea fedha fungu maalumu Ofisi ya Msajili wa Hazina ili iweze kulipa madeni ya serikali na kuziongezea mtaji kampuni na taasisi za Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akisoma maoni ya Kamati ya Bajeti, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Omary Kigua amesema licha ya Ofisi hiyo kupangia fedha kidogo katika mwaka wa fedha 2021/22, imepokea asilimia 54 tu hadi kufikia Aprili 2022.
Amesema ofisi hiyo ilipangiwa kupokea Sh 47 bilioni na hadi kufikia Aprili 2022 imepokea Sh. 25.4 bilioni, “kiasi hicho kilichotengwa mbali na kwamba kilikuwa kidogo ikilinganishwa na mahitaji imesababisha Serikali kutolipa madeni kikamilifu inayodaiwa na wananchi katika maeneo mbalimbali na kuwezesha taasisi zake kimtaji.”
Kigua amesema Kamati ya Bunge ya Bajeti inaona fungu maalum ni muhimu kwa ofisi kwasababu hutumika kurekebisha mitaji kwa mashirika ya umma yenye changamoto ya mitaji pamoja na kulipa madeni ya serikali iliyorithi kutoka CHC.
Pia amesema Kamati inaishauri Serikali kuiwezesha Ofisi ya Msajili wa Hazina kifedha ili iweze kutoa mitaji kwa makampuni na taasisi za umma kama vile Benki ya Kilimo na Benki ya Uwekezaji “ili ziweze kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Kamati inaamini kuwezesha ofisi hii ni kuongeza mapato ya Serikali yasiyotokana na kodi.”
Leave a comment