HALMASHAURI ya wilaya ya Mbozi mkoani Songwe imeeleza dhamira yake ya kuomba kupandishwa hadhi kuwa manispaa pamoja na kupatikana majimbo matatu, kwamba ni kuongeza ufanisi wa kuwatumikia wananchi. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe… (endelea).
Akizungumza na MwanaHALISI Online mwishoni mwa wiki, Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, George Msyani amesema wilaya hiyo yenye majimbo mawili ya Mbozi na Vwawa ina sifa zote za kuwa manispaa pamoja na nyongeza ya jimbo moja la Iyula kutokana na ukubwa wa halmashauri hiyo pamoja na idadi ya watu 510,599.
Amesema Kata za Idiwili, Kilimampimbi, Ukwile, Nyimbili, Hezya, Lwanda, Mahenje na Nanyala zitakuwa ndani ya jimbo jipya la Iyula huku jimbo la Vwawa na Mbozi yatabaki kama yalivyo na kuongeza chachu ya uwajibikaji na kuwatumikia wananchi.
Hayo yanajiri ikiwa ni wiki chache zimepita tangu Mbunge wa Vwawa, Japhet Hasunga naye kufikisha kilio hicho kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipokuwa kwenye ziara ya kikazi mkoani Songwe.
Mbozi ambayo inakusanya mapato ya Sh bilioni nne kwa mwezi ambayo Majaliwa alisema ni kiduchu, pia aliwataka viongozi wa halmashauri hiyo kuupanga mji huo na kuondokana na ujenzi holela.
Wilaya ya Mbozi ni moja ya wilaya kongwe nchini ambayo inategemea kukusanya mapato yake kupitia vyanzo mbalimbali ikiwemo kilimo cha mazao ya kahawa na parachichi.
Leave a comment