JIMBO la Hai linaloongozwa na Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), limetikiswa tena. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Ni baada ya wenyeviti wa vitongozi 13 wa chama hicho kujivua nyadhifa zao na kutimikia Chama Cha Mapinduzi (CCM), leo tarehe 18 Aprili 2019.
Hayo yanatokea ikiwa ni baada ya tarehe 6 Septemba mwaka jana, wenyeviti wa serikali za vijiji 19 wa Chadema kujivua nyadhifa zao, na kutimkia CCM.
Yohana Sintoo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Hai akizungumza na waandishi wa habari leo, amekiri kupokea barua za wenyeviti hao kujivua uanachama wa Chadema na madaraka yote.
Sintoo amewataja wenyeviti waliojiuzulu na kupokea barua zao kuwa ni Filbert Usiri (Nkwamandaa-Nronga), Eliatosha Lema (Maaseni-Nronga), Majisia Paul (Ngulujuu-Chemka), Nimkaza Mhando (Kikuletwa-Chemka), Gasper Mwasha (Boma Kati-Kware), Walter Swai (Masamu-Uswaa) na Majinsi Nyange (Lembeni A-Rundugai).
Pia Gladson Swai (Bomani), Ruyandumi Kimaro (Makiweru-Uswaa), Beda Msofe (Lembeni B-Rundugai), Ndemael Massawe (Nure-Ng’uni), Leonard Urassa (Njoro Chini-Shirinjoro) na Raymond Mushi (Nkwelengy-Nronga).
Sintoo amesema, baada ya kupokea barua hizo na kujiridhisha, uchaguzi wa kujaza nafasi hizo utafanyika Oktoba mwaka huu.
Kwa pamoja, wenyeviti hao baada ya kutangaza kuachana na Chadema, walikwenda kwenye Ofisi za CCM Wilaya ya Hai. Huko walipkewa na Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya hiyo, Wang’uba Magai pamoja na wajumbe wa kamati ya siasa ya wilaya hiyo.
Baada ya kupokea ‘wageni’ hao, Magai amesema, Mbowe anapaswa kujitathmini kama anafaa kuongoza jimbo hilo kwa kuwa, wasaidizi wake wameamua kuachana naye.
Leave a comment