SHAHIDI wa upande wa mashitaka katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amedai kuwa kiongozi huyo alibeba mawe ili kuwashambulia polisi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Shaban Khassan Abdallah, ameeleza kuwa, alimuona Mbowe na washitakiwa wengine tisa, wakiwa na mawe mkononi na marungu kwa lengo la kuwashambulia polisi.
“Niliwaona wakiwa na mawe na virungu. Walikuwa wakitembea barabarani huku wakiimba. Watuuwe, watuuwe, hatutoki mpaka mmoja wetu afe,” ameeleza Abdallah.
Ameongeza: “Hawa watu walikuwa wamejiandaa kwa shari kweli kweli. Niliweza kuwatambua Mbowe, Halima Mdee, Esther Matiko na John.”
Hakufafanua kama ni John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini au John Mnyika, Mbunge wa Kibamba.
Abdallah, shahidi wa pili katika kesi hiyo ya jinai inayomkabili Mbowe na viongozi wenzake wanane, alikuwa akiongozwa katika kutoa ushahidi wake na wakili mkuu wa serikali, Peter Kadushi leo tarehe 14 Mei 2019.
Amesema, anakumbuka kuwa siku ya tukio hilo alikuwa katika eneo la Mkwajuni, Kinodoni, Dar es Salaam na kushuhudia Mbowe na wenzake, wakiwa wamebeba mawe na walipanga kuwashambulia polisi na wananchi wengine.
Hata hivyo, shahidi huyo alipohojiwa na mawakili wa upande wa utetezi wakiongozwa na Peter Kibatala, alianza “kujikanyaga,” hasa katika eneo la shule aliyosoma.
Awali Abdallah ameeleza mahakama kuwa, alipata elimu yake ya sekondari katika Shule ya Msasani, iliyopo mkoani Kilimanjaro.
Leave a comment