JAMES Mbatia, aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, amesema Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, haiwezi kushughulikia mchakato wa upatikanaji katiba mpya, akidai haina uwezo wa kutekeleza jukumu hilo. Anaripoti Isaya Temu, TUDARCo…(endelea).
Mbatia ametoa kauli hiyo leo Jumamosi, tarehe 5 Agosti 2023, nyumbani kwake Mbezi Beach, jijini Dar es Salaam, akihojiwa na MwanaHALISI Online, kuhusu hali ya kisiasa iliyopo nchini.
Alipohojiwa kama ofisi hiyo inaweza ikafanikisha upatikanaji wa katiba mpya, Mbatia alidai ni kupoteza muda kwa kuwa haina rasilimali za kutosha ikiwemo watu na fedha kwa ajili ya kufanikisha zoezi hilo.
“ Unajua suala la katiba ni uhai wa taifa, ofisi ya Msajili wa vyama vya Siasa iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, na huyo Msajili wa Vyama vya Siasa yuko chini ya Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu yaani ni kakitengo kadogo Mno,” amesema Mbatia.
Mbatia ameuita mchakato huo unaondelea hivi sasa, ni majanga kwani hauwezi kukamilika.
“ Waliomshauri Mheshimiwa Rais kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa asimamie mchakato wa Katiba ni kichekesho, kwa kweli hatutapata na mtaona tu na hili ninaliongelea kimajanga majanga, ni janga lingine pia kwa sababu tunaendelea kupoteza muda kusema kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa atatupa katiba mpya haitawezekana,”amesema Mbatia.
Haya ameyaongea baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Samia Suluhu Hassan, kumpatia jukumu Msajili wa vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, la kusimamia mchakato wa katiba mpya ambao umeonekana kusuasua.
Leave a comment