MBUNGE Viti Maalum (CCM), Fakharia Shomar Khamis, ameihoji Serikali kama inafahamu watumiaji wa dawa za kulevya ‘Mateja’, wanaongoza kwa vitendo vya wizi wa vyuma, kufuatia kushamiri kwa biashara ya vyuma chakavu nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Fakharia amehoji hayo leo Jumatano, tarehe 9 Juni 2021, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
“Kwa kuwa baadhi ya wengi wanaohujumu vyuma chakavu wengi wao wanatumia vilevi, ambavyo havikubaliki kwa jamii mfano wala unga, ambao ndiyo jamii kubwa inayofanya kazi hizo za kubeba vyuma chakavu. Serikali suala hili inalijua na kama inalijua imeliangaliaje?” Amehoji Fakharia.
Wakati huo huo, Fakharia amehoji mkakati wa Serikali katika kukabiliana na wizi wa vyuma, ikiwemo kuanzisha sheria maalum itakayodhibiti biashara ya vyuma chakavu, inayochangia kukithiri kwa wizi huo.
“Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na wizi wa vyuma unaosababishwa na kushamiri kwa biashara ya chuma chakavu nchini. Je, Serikali haioni kwamba biashara ya vyuma chakavu ni hatarishi hata kwa usalama wa raia na mali zao?” Ameuliza Fakharia.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi na Vijana, Jenista Mhagama, amesema Serikali kupitia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), imekuwa ikiwatafuta waathirika wa dawa za kulevya.
Kwa ajili ya kuwapeleka katika vilabu vinavyowapatia msaada wa kuachana na matumizi hayo.
“Ni kweli kabisa wengi kati ya vijana ambao wamekuwa wakijihusisha na shughuli hiyo, wamekuwa na dalili za viashiria vya matumizi ya dawa za kulevya za aina mbalimbali,” amesema Mhagama na kuongeza:
“Mamalaka ya kupambana na matumizi ya dawa, inachofanya kuanzisha klabu katika mitaa na shule, kubaini hata hao vijana wanaojiusha na shughuli hizo na nyingine, lengo kuwasaidia kuwaondoa huko na kuacha kujihusisha na matumizi ya dawa za kulevya.”
Kuhusu wizi wa vyuma, Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Hamad Chande, amesema Serikali imeweka sheria na kanuni mbalimbali kwa ajili ya kudhibiti wizi wa vyuma katika miundombinu mbalimbali.
“Serikali imekuwa ikifanya ufuatiliaji ili kudhibiti hujuma ya miundombinu ya Serikali na watu binafsi. Aidha, wananchi na vyombo mbalimbali vinaombwa kushiriki pamoja katika kulinda miundombinu dhidi ya watu waovu na wasio wazalendo,” amesema Chande.
Leave a comment