WAZIRI wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba amekabidhiwa ofisi rasmi na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Dk. Stergomena Tax katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Waziri Makamba amemshukuru Dk. Tax kwa ushirikiano aliompatia wakati wote tangu yalipofanyika mabadiliko ya Baraza la Mawaziri mwishoni mwa mwezi Agosti 2023.
“Tangu Mheshimiwa Rais alipofanya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri umekuwa ukinipatia ushirikiano wakati wote, nakushukuru sana, pia nakutakia heri katika majukumu yako mapya” amesema Waziri Makamba
Naye Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Tax amesema alipohudumu katika Wizara hiyo alipata ushirikiano mkubwa kutoka kwa menejimenti na watumishi wa Wizara na kumhakikishia Waziri Makamba kuwa ana watumishi wachapakazi
“Wakati wa utumishi wangu hapa wizarani, nilipata ushirikiano mkubwa, hivyo napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru sana menejimenti na watumishi wote wa wizara kwa ushirikiano walionipa,” alisema Dk. Tax
Amesema jukumu lililo mbele ya Wizara hiyo ni kutekeleza maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa vitendo kwa kutafuta fursa mbalimbali za kukuza uchumi na kuendeleza diplomasia ya uchumi
Pamoja na mambo mengine, Dk. Tax pia amemtakia utendaji kazi mwema Waziri Makamba na kuwashukuru Naibu Waziri Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Katibu Mkuu Mkuu wa Wizara, Balozi Dk. Samwel Shelukindo, Naibu Katibu Mkuu, Menejimenti na watumishi wa Wizara.
Makabidhiano hayo yalihudhuriwa pia na wajumbe wa menejimenti na baadhi ya watumishi wa wizara.
Leave a comment