MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam (RC), Amos Makalla amemuagiza Kamanda mpya wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro kuhakikisha anakomesha uhalifu mkoani humo. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Muliro amehamishiwa mkoani humo hivi karibuni akitoka Mkoa wa Mwanza kwa nafasi hiyo hiyo na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro.
Kamanda Muliro amechukua nafasi ya Kamishna Camilius Wambura ambaye aliteuliwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).
Makalla ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa huo, amekutana na Kamanda Muliro, ofisini kwake leo Jumanne, tarehe 8 Juni 2021.
Makalla amemuelekeza Kamanda Muliro kuendelea na operesheni ya kuwashughulikia kikamilifu majambazi na wahalifu mkoani humo ili Dar es Salaam ibaki kuwa tulivu na wananchi wafanye shughuli zao kwa usalama.
Aidha Makalla amesema, kwa sasa hali ya usalama Dar es Salaam ni shwari na hataki kusikia majambazi yakifanya uhalifu.
Leave a comment