MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa amesema kiti cha urais siyo cha mchezo, kinahitaji mtu makini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kwimba … (endelea).
“Uongozi wa nchi siyo jambo la mchezo, linataka kiongozi makini, kiongozi anayetetea rasilmali na anayetetea wanyonge dhidi ya rushwa na ufisadi,” amesema.
Majaliwa ametoa kauli hiyo jana mchana Alhamisi tarehe 24 Septemba, 2020 wakati akizungumza na wakazi wa kata za Hungumalwa na Ngudu wilayani Kwimba, mkoani Mwanza kwenye mkutano uliofanyika kwenye viwanja vya sokoni.
“Wengine watakuja kuomba kura lakini kazi yao kubwa ni kukashifu kila jambo linalofanywa na Serikali. Naomba kura za wananchi wote, wana CUF, Chadema, ACT mkipigie kura Chama Cha Mapinduzi sababu maendeleo hayana chama.”
“Wakija hapa muwasikilize; mkiwauliza Ilani yao watakwambia wanayo ila iko kwenye website. Sisi ya kwetu tunayo hii hapa,” alisema huku akionesha Ilani ya CCM ya 2020 – 2025.”
Aliwataka wakazi hao wafanye maamuzi thabiti ya kutafuta viongozi tena wanaozungumza lugha moja.
“Viongozi hao ninawaombea kura ni Rais, Mbunge na Diwani. Msichague viongozi ambao kazi yao ni kusema hapana kwenye mambo ya maendeleo au kwenye bajeti ya Taifa. Naomba kura kwa viongozi hao watatu,” alisema.
Majaliwa ambaye yuko mkoani Mwanza kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, John Pombe Magufuli, alitumia fursa hiyo kumwombea kura mgombea ubunge wa Kwimba, Shanif Mansoor, mgombea udiwani wa Hungumalwa, Bukaba Majoge na madiwani wa kata zote za wilaya ya Kwimba.
Wakati huohuo, mgombea ubunge wa Geita Vijijini, Joseph Kasheku Msukuma ambaye aliwepo kwenye mikutano huo, alitumia fursa hiyo kuiomba Serikali iwajengee soko la kisasa wakazi wa Hungumalwa kwa sababu eneo hilo pana biashara kuwa ya dengu, choroko na kunde.
Leave a comment