MAALIM Seif Shariff Hamad, mgombea urais visiwani Zanzibar kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, amesema safari hii vijana wapo tayari. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
“Tunapambana na CCM (Chama Cha Mapinduzi) na nafikiri vijana wengi safari hii wamejipanga na kujiandaa, likitokea lolote wapo tayari,” amesema Maalim Seif wakati akizungumza na gazeti moja la kila wiki, mapema wiki hii.
Akizungumzia ushindani uliopo kati yake na CCM, amesema ndani ya chama hicho, wapo wanaomuunga mkono kutokana na kutoridhishwa na mgombea aliyeteuliwa na chama hicho.
Mgombea aliyeteuliwa na CCM kugombea urais Zanzibar NI Dk. Hussein Ali Mwinyi na kwamba, anajua hapambani na Dk. Mwinyi pekee bali CCM wote.
“Tofauti iliyopo baina ya chaguzi zote hizo ni ndogo sana, kwa sababu chaguzi zote hizi tunashindana na wagombea wa CCM. na CCM ni ile ile na kwa kweli unaposhindana na CCM hushindani na mgombea, unashindana na CCM wote.
“…tofauti iliyopo kubwa hivi sasa ndani ya CCM , hakuna ule umoja ambao walikuwa nao zamani. Watu wengi sasa hivi hawaridhishi na mgombea aliyeletwa na chama chao kuwania nafasi hiyo,” amesema Maalim Seif.
kwa hiyo, kidogo inatufanya tuamini kwamba kuna watu wengi wanaotuunga mkono ndani ya CCM.
Akizungumzia kauli ya kwamba yeye ni ‘mgombea mzoefu wa kushindwa’ amesema yeye si mzoefu wa kushindwa bali mzoefu wa kudanganywa.
“…sidhani kama mimi ni mzoefu wa kushindwa, lakini mimi ni mzoefu wa kudanganywa, kuanzia mwaka 1995, 2000, 2005, 2010 na hata 2015 nimekuwa nikishinda na ushahidi kamili ulipatikana mwaka 2015.
“Na hii kila mmoja alijua kama tumeshinda tena kwa kura nyingi sana, lakini mwenyekiti wa tume akapata maagizo ya kuwa afute uchaguzi kinyume cha Katiba na sheria, kwa hiyo kwamba nashindwa aaaah! nanyang’anywa,” amesema.
Leave a comment