SAED Kubenea, mgombea ubunge Kinondoni, jijini Dar es Salaam kupitia Chama cha ACT-Wazalendo amesema, miongoni mwa mambo atakayosimamia ni kuhakikisha linaundwa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF), lisilokuwa na viongozi mashabikiwa wa vilabu vikubwa vya mpira nchini. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Amesema, shirika hilo ambalo litaundwa kwa mijibu wa Bunge, litasimamia michezo kwa haki na usawa.
Ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Mzimuni iliyopo ndani ya jimbo hilo, wakati akiendelea na kampeni zake za mtaa kwa mtaa.
“Ukiwa na chama cha soka kinachosimamia michezo, ndani yake mkileta ushabiki wa Yanga na Simba, mpira hautaendelea. Tunataka watu ambao wakifika TFF, Simba na Yanga waziache nyumbani kwao, pale wakasimamie timu zote kwa kuwa wao ndio wasimamizi wa mpira wetu,” amesema Kubenea.

Pia ameahidi wananchi wa Kinondoni kwambwa, atahakikisha anawapa mikopo wafanyabiashara, kupunguza kodi na huku wafanyabiashara ndogondogo hawalipi kodi kubwa hadi wanapokuwa na kiwango cha wafanyabiashara wa kati.
Amesema, ana mpango wa kanzisha shule za sekondari za kidato cha tano na sita ndani ya jimbo hilo kwa kuwa, hazipo kwa sasa.”Tunataka kuimarisha vituo vya afya na hospitali za umma, kuhakikisha dawa zinapatikana na mtu aliyetimiza miaka 60 anahudumiwa bure.
“Tunataka mtu akifa katika hospitali ya serikali, mwili wa marehemu usizuiwe kwenda kuzikwa mpaka ulipiwe bili, aliyefiwa alipe akazike ndugu yake,” amesema.
Kubenea anaendelea kufanya kampeni za mtaa kwa mtaa katika maeneo mbalimbali ya jimbo hilo ikiwa ni pamoja na kuwatembelea waliokumbwa na maafa ya mafuriko kwenye Bonde la Mto Msimbazi.
Leave a comment