MAALIM Seif Sharif Hamad, mgombea urais visiwani Zanzibar kupitia Chama cha ACT-Wazalendo amesema, Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), hana ubavu wa kumfanya chochote. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Amesema, ikiwa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, Mwenyekiti wa kwanza wa chama hicho hakuweza kumchukulia hatua “yeye ataweza wapi?”
“Polepole eti anatisha mie kwamba Seif ‘stop’ au tutamchukulia hatua, ikiwa Mwalimu Julius Nyerere hakunifanya kitu, kaniacha hapa hapa itakuwa Polepole? “ amehoji Maalim Seif.
Kauli hiyo ameitoa jana Alhamisi tarehe 17 Septemba 2020, katika mkutano wa kampeni kwenye Viwanja vya Mbuzini Skuli visiwani Zanzibar.
Ni baada ya Polepole, mwishoni mwa Agosti 2020 kudai, kwamba Maalim Seif anachafua viongozi wa chama hicho na kwamba akiendelea, atamshughulikia.
Polepole alitoa kauli hiyo wakati akitaja orodha ya wagombea uwakilishi Zanzibar kupitia CCM, ambapo alimuita Maalim Seif mzee.
Maalim Seif ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo, amesema “Polepole anasema CCM kinawaletea kijana mbichi na atabadilisha Zanzibar na sio mzee ambaye anastahiki kukaa kuwalea wajukuu, sasa namwambia nina wajukuu na wa kwanza yeye Polepole, Polepole mimi ni babu yako unastahiki ufunzwe.”
Maalim Seif amesema, Polepole hajui mila na desturi za Wazanzibar ya kwamba, mtoto anapaswa kuwaheshimu wazee kama yeye, hivyo ni vema akaenda kwake ili amlee.
“Wewe masikini ya Mungu hujui desturi, mila wala silka za Wazanzibari, leo mtoto kama wewe mdogo anaweza kuja akatukana wazee? Wazee wanasikitika tu, Polepole njoo nikulee nikufundishe maadili ya Kizanzibari,” amesema Maalim Seif.
CCM imemsimamisha Dk. Hussein Ali Mwinyi kuwa mgombea urais visiwani humo katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika tarehe 27 na 28 Oktoba 2020, ambapo Polepole alisema mgombea huyo ni kijana na damu changa, hivyo anayefaa kuongoza Wazanzibar.
Leave a comment