Friday , 26 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Maalim Seif: Hakuweza Nyerere, itakuwa Polepole?
Habari za Siasa

Maalim Seif: Hakuweza Nyerere, itakuwa Polepole?

Spread the love

MAALIM Seif Sharif Hamad, mgombea urais visiwani Zanzibar kupitia Chama cha ACT-Wazalendo amesema, Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), hana ubavu wa kumfanya chochote. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).

Amesema, ikiwa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, Mwenyekiti wa kwanza wa chama hicho hakuweza kumchukulia hatua “yeye ataweza wapi?”

“Polepole eti anatisha mie kwamba Seif ‘stop’ au tutamchukulia hatua, ikiwa Mwalimu Julius Nyerere hakunifanya kitu, kaniacha hapa hapa itakuwa Polepole? “ amehoji Maalim Seif.

Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),

Kauli hiyo ameitoa jana Alhamisi tarehe 17 Septemba 2020, katika mkutano wa kampeni kwenye Viwanja vya Mbuzini Skuli visiwani Zanzibar.

Ni baada ya Polepole, mwishoni mwa Agosti 2020 kudai, kwamba Maalim Seif anachafua viongozi wa chama hicho na kwamba akiendelea, atamshughulikia.

Polepole alitoa kauli hiyo wakati akitaja orodha ya wagombea uwakilishi Zanzibar kupitia CCM, ambapo alimuita Maalim Seif mzee.

Maalim Seif ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha ACT-Wazalendo, amesema “Polepole anasema CCM kinawaletea kijana mbichi na atabadilisha Zanzibar na sio mzee ambaye anastahiki kukaa kuwalea wajukuu, sasa namwambia nina wajukuu na wa kwanza yeye Polepole, Polepole mimi ni babu yako unastahiki ufunzwe.”

Maalim Seif amesema, Polepole hajui mila na desturi za Wazanzibar ya kwamba, mtoto anapaswa kuwaheshimu wazee kama yeye, hivyo ni vema akaenda kwake ili amlee.

“Wewe masikini ya Mungu hujui desturi, mila wala silka za Wazanzibari, leo mtoto kama wewe mdogo anaweza kuja akatukana wazee? Wazee wanasikitika tu, Polepole njoo nikulee nikufundishe maadili ya Kizanzibari,” amesema Maalim Seif.

CCM imemsimamisha Dk. Hussein Ali Mwinyi kuwa mgombea urais visiwani humo katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika tarehe 27 na 28 Oktoba 2020, ambapo Polepole alisema mgombea huyo ni kijana na damu changa, hivyo anayefaa kuongoza Wazanzibar.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

error: Content is protected !!