MWENYEKITI wa Chama cha ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad ameweka bayana msimamo wake wa kumuunga mkono Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu uko palepale na “hakuna mwingine zaidi ya Lissu.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
Akizungumza katika mkutano wa kampeni wa Lissu uliofanyika jana Jumatatu tarehe 19 Oktoba 2020 kwenye Jimbo la Moshi Mjini mkoani Kilimanjaro, Maalim Seif alisema anamuunga mkono Lissu.
Maalim Seif ambaye ni mgombea urais wa Zanzibar kupitia ACT-Wazalendo amewaomba wafuasi wake wa Tanzania Bara na Zanzibar kumpigia kura ya ndio Lissu katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Zaidi ya mara moja Maalim Seif ametamka hadharani kumuunga mkono Lissu badala ya kumuunga mkono Mgombea Urais wa chama chake cha ACT-Wazalendo, Bernard Kamilius Membe.
Soma zaidi:-
Mwanasiasa huyo alisema, sababu ya kumuunga mkono Lissu ni ujasiri wake na dhamira yake ya kutetea masilahi ya Watanzania.
“Madhumuni yangu kuwaambia Watanzania kwamba, mimi Maalim Seif namuunga mkono Lissu, wale wote ambao wananifuata mimi Bara na Zanzibar kura kwa Tundu Lissu.”
“Katika wagombea wote wa Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hakuna mwingine kuliko Lissu, ni jasiri sana,” alisema Maalim Seif huku akishangiliwa na umati wa watu wananchi kwenye mkutano huo.
Maalim seif amesema, Wazanzibar hawana mashaka na Lissu kwani wanaamini akishinda Urais wa Tanzania ataimarisha muungano.
“Mimi naamini kabisa, Mungu amlinde Lissu sababu kuna kazi maalum Mungu kamtengenezea nayo ni rais, sisi Wazanzibar hatuna wasiwasi na Lissu. Akiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Maalim Seif akiwa Zanzibar tutaleta muungano wa haki sio muungano wa kughushi,” alisema.
“Sisi tutawaunganisha kweli Watanzania wa Bara na Zanzibar kufikia muungano wa nchi mbili zilizo sawa na haki, ambao kila sehemu itamheshimu mwenzake. Ombi langu kura zenu zote kwa Lissu,” alisema Maalim Seif.
Msimamo huo wa Maalim Seif umekuja saa kadhaa baada ya Membe kuibuka baada ya ukimya kirefu na kusema, yeye bado mgombea halali wa chama hicho.
Membe alitoa kauli hiyo jana Jumatatu wakati anazungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam ambapo alisema, atatumia siku chache zilizosalia kufanya kampeni za kishindo huku akiahidi kupata ushindi.
Mwanasiasa huyo alisema, misimamo inayotolewa na viongozi wa juu wa ACT-Wazalendo kumuunga mkono Mgombea wa Chadema ni msimamo wao binafsi, bali chama chake kinaendelea kumtambua kama mgombea halali wa urais.
Mbali na Maalim Seif, Kiongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe naye alitamka hadharani kumuunga mkono Lissu na atampigia kura Lissu kwani anafaa kuwa Rais wa Tanzania.
Leave a comment