Friday , 3 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Luteni Urio: Sikuamini kama Mbowe anaweza kufanya ugaidi
Habari za SiasaTangulizi

Luteni Urio: Sikuamini kama Mbowe anaweza kufanya ugaidi

Spread the love

 

ASKARI wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Luteni Denis Urio, amedai hakuamini kama Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, anaweza kufanya vitendo vya kigaidi kwa kuwa hana historia hiyo, lakini baadae alibaini kwamba alikuwa amedhamiria. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Luteni Urio ametoa madai hayo leo Jumatatu, tarehe 31 Januari 2022, akitoa ushahidi wake katika kesi ya uhujumu uchumi namba 16/2021, inayomkabili Mbowe na wenzake watatu, katika Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, mbele ya Jaji Joachim Tiganga.

Ni baada ya Wakili wa utetezi, Peter Kibatala kumhoji kwa nini hakuieleza mahakama hiyo tarehe ambayo Mbowe alimueleza nia yake ya kupanga njama za kufanya vitendo vya kigaidi.

Na tarehe ambayo aliripoti njama hizo kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa  Makosa ya Jinai nchini (DCI) Robert Boaz na aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Arusha (RCO), ACP Ramadhan Kingai.

Ambapo Luteni Urio alijibu akidai hakumbuki.

Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni waliokuwa makomando wa JWTZ, Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdillah Ling’wenya, ambao wanakabiliwa na mashtaka sita ya ugaidi, ikiwemo kutaka kudhuru viongozi wa Serikali walioonekana kikwazo kwa vyama vya siasa vya upinzani.

Mahojiano kati ya Wakili Kibatala na Luteni Urio yalikuwa kama yafuatavyo;

Kibatala: Ni kweli kwamba matukio haya ya kukutana na mtu ambaye ulikuwa na uhusiano naye wa karibu akakwambia mipango ya kufanya vitendo vya ugaidi, ni kitu kizito kimetokea mara ya kwanza katika maisha yako ya utumishi wa umma?

Shahidi: Kuambiwa sijawahi

Kibatala: Utakubaliana na mimi ni kitu fulani kina uzito wa kipekee katika maisha yako?

Shahidi: Sahihi kina uzito wa kipekee

Kibatala: Nakumbuka ulitoa ushahidi kwamba  hauna matatizo yoyote ya kumbukumbu?

Shahidi: Sina matatizo yoyote ya kumbukumbu

Kibatala: Shahidi naomba utusaidie, inawezekana vipi usikumbuke tarehe za muhimu mbili ambazo ziko central kwenye suala lote hili.

Tarehe mahususi ya kuongea na Mbowe akakwambia mambo mazito na tarehe ya kwenda ofisini kwa DCI  kumpa taarifa nzito namna hii, inakuwaje unashindwa kukumbuka?

Shahidi: Mheshimiwa  Jaji kwanza Mbowe namfahamu, lakini sikuamini anaweza kufanya kitu kama hicho, ndio maana nikaenda kuripoti polisi inawezekana kweli au  si kweli, na-asume anaweza kufanya kweli, nilipojiridhisha nilijua ilikuwa serious

Kibatala: Jibu swali langu inawezekana matukio kama haya huwezi kukumbuka?

Shahidi: Sijawahi kusikia matukio hayo, ndio maana nikaenda kuripoti kama kufanya uchunguzi polisi wakafanya uchunguzi, ndio ukamataji ukaendelea

Kibatala: Inawezekana vipi ushindwe kukumbuka matukio muhimu kama hayo?

Shahidi: Mara ya kwanza kupata taarifa kama hizo kwa Mbowe sikuamini kama kitatokea kitu kama hicho, nikaripoti, kama kungekuwa na historia nyingine au kuwa na rekodi ningeamini, lakini hana rekodi hiyo

Kibatala: Kuripoti DCI  ni tarehe muhimu kwa nini hukumbuki?

Shahidi: Siwezi kukumbuka sababu sio duty yangu  kupeleleza, mimi nilienda kutoa taarifa ya uhalifu

Kibatala: Unaweza kueleza kwa nini hata DCI katika maelezo yake kwenye bando la Committal  hafahamu tarehe mahususi?

Shahidi: Sifahamu

Kibatala: Kwa nini hata ACP  Kingai katika maelezo yake naye hakumbuki tarehe mahususi ambayo wewe umeenda ripoti kwa DCI, unaweza tusaidia kujua ni kwa nini?

Shahidi: Sijui kwa nini

Kibatala: Kwa nini pia Inspekta Swilla ambaye maelezo yake tumepewa naye hakumbuki tarehe mahususi, isipokuwa tarehe ya kufungulia kesi 18 Julai 2020, unaweza fahamu kwa nini?

Shahidi: Sifahamu

Kibatala: Hii hali Luteni unaiona ya kawaida? Wewe hukumbuki uliyeenda kuripoti kwake, DCI hakumbuki, ACP Kingai hakumbuki, Inspekta Swilla aliyekufanyia upelelezi na kuchukua simu zako hakumbuki, unaona ni hali ya kawida?

Shahidi: Siwezi kujibia chombo cha polisi

Kibatala: Unaona ni hali ya kawaida?

Shahidi: Nimeenda kwenye ofisi ya mtu suala la ku-take note, kutoku-take note siwezi kumlazimisha

Kibatala: Kwa nini kama kweli Inspekta Swilla anavyodai alifungua faili  tarehe 18 Julai la tuhuma za kula njama za kufanya vitendo vya ugaidi, shtaka linalohusisha zaidi ya mtu mmoja, unaweza kutusaidia kwa nini alisubiri mpaka angalau mwezi mmoja baadae tarehe 11 Agosti 2020 aliandika maelezo yako ambayo yalitumika kuanzisha jalada, unafahamu kwa nini maelezo yako yamekuja kundikwa tarehe 11 Agosti 2020?

Shahidi: Sifahamu

Kibatala: Katika hali ya kawaida sababu sio afisa wa polisi ni mtu mwenye upeo fulani, sio kitu cha busara na ambazo kinategemewa kwa watu  wanaofahamu majukumu yao kurekodi taarifa za uhalifu mapema iwezekanavyo, nataka tathmini yako, huoni kwamba inategemea maelezo ya mtu muhimu kama mtoa taarifa yaandikwe mapema?

Shahidi: Sifahamu sababu ni taasisi mbili tofauti, ataandika muda gani ni juu yake yeye

Luteni Urio anaendelea kutoa ushahidi wake mahakamani hapo.

Katika ushahidi wake mkuu, Luteni Urio alidai Julai 2020 alikutana na Mbowe kisha mwanasiasa huyo akamuomba amtafutie makomando wa JWTZ waliofukuzwa ama kustaafu jeshini, ili wamsaidie katika harakati za chama chake kuchukua dola kwa gharama yoyote.

Ikiwemo kuzua taharuki kwa jamii kwa kuchoma vituo vya  mafuta na kulipua maeneo yenye mikusanyiko ya watu, kukata miti iliyoko maeneo ya barabarani na kupanga magogo barabarani.

Luteni Urio anadai aliripoti njama hizo za Mbowe kwa DCI Boaz ambapo alimuelekeza atekeleza ombi la mwanasiasa huyo la kumtafutia makomando kisha aripoti mwenendo wake kwa ACP Kingai.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Sabaya afutiwa kesi, ruksa kugombea uongozi

Spread the loveMwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali DPP leo Ijumaa amefuta rufaa...

Habari za Siasa

Serikali yasaka bilioni 3 kujenga daraja Mto Mpiji

Spread the loveSerikali imesema inaendelea na juhudi za kutafuta fedha kiasi cha...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema kwafukuta kisa chaguzi, Lissu aibua tuhuma nzito

Spread the loveCHAGUZI za kusaka viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo...

Habari MchanganyikoTangulizi

Kimbunga “HIDAYA” chaendelea kuimarika, wananchi wapewa tahadhari

Spread the loveMAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inaendelea kutoa taarifa...

error: Content is protected !!