Saturday , 27 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Lowassa, Sumaye wamtia gundu Membe
Habari za Siasa

Lowassa, Sumaye wamtia gundu Membe

Spread the love

WASWAHILI husema ‘ukiumwa na nyoka, ukigusa jani unashtuka,’ hiki ndicho kinachomtokea Bernard Membe, Waziri wa Mambo ya Nje katika serikali ya awamu ya nne. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).

Hatua ya Edward Lowassa na Frederick Sumaye, mawaziri wakuu wastaafu kutoka chama cha upinzani – Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) – na kurejea Chama Cha Mapinduzi (CCM), imemtia nuksi na kumweka kwenye wakati mgumu Membe.

James Mbatia, Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi anaungana na vyama vingine, kuonesha hofu ya kumpokea Membe iwapo atataka kujiunga na chama hicho.

Akizungumza na wahariri waandamizi wa Kampuni ya Mwananchi Communication (CML), jijini Dar es Salaam leo tarehe 10 Machi 2020, alipoulizwa kama chama chake kiko tayari kumpokea Membe iwapo atataka kujiunga na nacho, Mbatia amesema lazima kuwe na umakini.

Mbatia ameeleza wazi, kwamba kilichofanywa mwaka 2015, wakati walipomkaribisha na kumruhusu Lowassa kujiunga na kisha kugombea urais, akiungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kinatakiwa kutotokea tena.

Amemtaja Lowassa na Sumaye kama mfano mbaya ambao wapinzani wanapaswa kujifunza, na kwamba ndio msingi wa kumuhofia Membe.

“Makosa ya 2015 ya kina Lowassa, Sumaye na wengine yawe mafundisho tosha kwetu sisi,” amesema Mbatia na kuongeza, kwamba kumpokea mtu na kuwa mwanachama, anakuwa na haki zote hivyo lazima umakini uwepo.

Lowassa alijiunga na Chadema Julai 2015, huku ikielezwa kwa masharti ya kuteuliwa na kugombea urais jambo ambalo lilitekelezwa na kuacha mpasuko mkubwa ndani ya vyama vya upinzani.

Lowassa alitangaza kurejea CCM tarehe 1 Machi 2019, ambapo Sumaye alitangaza kurejea kwenye chama hicho tarehe 10 Februari 2020.

Miongoni mwa wanaoonesha mashaka ya kumpokea Membe ni pamoja na Maalim Seif Sharif Hamad, Mshauri Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo.

Maalim Seif alisema, Membe kama anataka kujiunga na chama hicho, hapaswi kwenda na masharti kama ilivyotokea kwa Lowassa mwaka 2015.

Maalim Seif alisema “Membe? Sie tunapokea yeyote atakayekuja, asije na masharti, tunampokea.”

Mzee Hashimu Juma, Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la Chadema (BAZECHA), tarehe 3 Machi 2020 alisema Chadema kimeweka matumaini yake kwa Tundu Lissu, makamu mwenyekiti wa chama hicho kugomea urais kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.

Mzee Juma alimshauri Membe kujiunga na chama kingine cha upinzani ili kupunguza kura za CCM, huku akitamba kwamba hawezi kupunguza kura za Chadema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

ACT: Waongoza watalii wapate maslahi yao inavyostahili

Spread the loveCHAMA cha ACT-Wazalendo kimeitaka serikali kuhakikisha inasimamia maslahi stahiki ya...

Habari za SiasaTangulizi

Prof. Lipumba ajitosa kuviunganisha vyama vya siasa Burundi

Spread the love  MWENYEKITI wa Kituo Cha Demokrasia Tanzania (TCD), Prof. Ibrahim...

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

error: Content is protected !!