WAKILI Fatma Karume amemueleza Rais John Magufuli kwamba, yuko tayari kukaa jela miaka 30, ili kuboresha demokrasia na utawala wa sheria nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Fatma ametoa kauli hiyo jana tarehe 20 Septemba 2019 kupitia ukurasa wake wa Twitter, saa kadhaa baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kumsimamisha uwakili kwa muda ikimtuhumu kutoa kauli za kuishambulia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
“Nimemalizika kwa kunifungia uwakili?Nyinyi mnaendeshwa kwa njaa ya matumbo yenu na si njaa ya haki! Mwambieni Rais Magufuli niko tayari kufa kwa Demokrasia na Utawala wa Sheria. Wasiojulikana wanajua nakaa wapi waje tu,” amesema Fatma.
Fatma aliyewahi kuwa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) amesema kitendo cha kusimamishwa uwakili, hakitoshi kulipia thamani ya demokrasia na utawala wa sheria.
“Rais Magufuli nataka uelewe niko tayari kukaa jela miaka 30 kama kukaa kwangu jela italeta demokrasia na utawala wa sheria nchi hii.Kwa hivyo kuchukua haki yangu ya kusimamia sheria ni bei ndogo sana kulipia itikadi muhimu kama Demokrasia na utawala wa Sheria,” amesema Fatma
Jana, Mahakama Kuu iliamuru Fatma asiendelee kuwa wakili kwa muda, kutokana na upande wa serikali kulalamikia matamshi aliyotoa katika kesi iliyofunguliwa na Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa ACT Wazalendo dhidi ya Rais Magufuli na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Leave a comment