MKURUGENZI wa Makosa ya Jinai (DPP), amekata rufaa kupinga kufutwa kwa makosa ya utakatishaji fedha katika kesi inayowakabili aliyekuwa Rais wa Klabu ya Simba, Evance Aveva na Godfery Nyange (Kabulu) kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Kwenye kesi hiyo, mshtakiwa mwengine kwenye kesi hiyo ni Zackaria Hanspopo ambapo leo tarehe 20 Septemba 2019, mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, Wakili wa Serikali Mwandamizi Wankyo Simon, ameieleza mahakama kuwa upande wa mashtaka umekata rufaa ya kupinga uamuzi uliotolewa jana tarehe 19 , Septemba 2019 mahakama hiyo.
Wankyo ameieleza mahakama hiyo kuwa, upande wa mashtaka haujajiandaa kutoa hoja juu ya rufaa hiyo, hivyo ameomba shauri hilo kutajwa siku nyengine.
Wakili wa utetezi Nehemia Nkoko amieleza mahakama hiyo kuwa upande huo, upo tayari na utetezi na kwamba wao walikuwa mahakamani hapo tangu asubuhi sambamba na mashahidi wao.
Nkoko ameeleza, upande wa Jamhuri ulikuwa na notisi ya rufaani tangu asubuhi wangeweza kuwasilisha hoja zao.
Ameeleza, uwa upande wa serikali haujapinga dhamana ya washtakiwa na kwamba ilishatolewa tangu jana.
Baada ya kusikiliza pande zote mbili, Hakimu Simba amesema kuwa misingi ya mahakama ni kusikiliza, na kwamba itakuwa haijautendea haki upande wa Jamhuri kwenye rufaa yao.
Amesema, atasikiliza hoja za upande huo siku ya Jumatatu tarehe 23 Septemba 2019, na kwamba hajafuta dhamana ya washtakiwa. Aveva na wenzake wamerejeshwa mahabusu.
Leave a comment