ALIYEKUWA Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake wawili, wamekutwa na kesi ya kujibu katika mshtaka ya unyang’anyi wa kutumia silaha, yanayowakabili kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Odira Amworo, imemkuta Sabaya na wenzake, Sylvester Nyegu na Daniel Mbura, wana kesi ya kujibu, leo Alhamisi, tarehe 12 Agosti 2021, baada ya mashahidi upande wa Jamhuri kutoa ushahidi wao mahakamani hapo.
Hivyo, imepanga kuanza kusikiliza utetezi wa washtakiwa hao kesho Ijumaa, tarehe 13 Agosti mwaka huu.
Sabaya na wenzake wanakabiliwa na mashtaka matatu katika kesi hiyo iliyofunguliwa mahakamani hapo Juni 2021, ambapo wanadaiwa kutenda makosa hayo tarehe 9 Februari 2021, kwenye duka la Mohamed Saad, lililoko eneo la Bondeni jijini Arusha.
Kwa mara ya kwanza, Sabaya na wenzake walifikishwa kizimbani tarehe 4 Juni 2021 na kusomewa mashtaka hayo.
Katika kesi hiyo, washtakiwa hao wanadaiwa kumfanyia unyang’anyi wa kutumia silaha, Diwani wa Sombetini (CCM), Bakari Msangi na kumuibia Sh. 390,000.
Pia, washtakiwa hao wanadaiwa kumpiga mateke na kumtishia silaha, Ramadhani Ayoub, kisha kumpora simu na Sh. 35,0000.
Leave a comment