SERIKALI ya Tanzania, imepanga kutumia Sh. 2.974 trilioni, kwa ajili kuongeza mtandao wa barabara za lami na changarawe, pamoja na ujenzi wa madaraja, katika kipindi cha miaka mitano (2021/22 hadi 2025/26). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Alhamisi, tarehge 12 Agosti 2021 na Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Ummy Mwalimu, akifungua mkutano wa wizara hiyo na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura), uliofanyika jijini Dodoma.
Ummy amesema, katika kipindi hicho cha miaka mitano, Serikali kupitia Tarura, itajenga barabara za kiwango cha lami zaidi ya kilomita 1,000, za changarawe kilomita 73,242 na madaraja 3,808.
“Serikali kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2021/22 hadi 2025/26, imepanga kuongeza mtandao wa barabara za lami kutoka kilometa 2,404.90 hadi kilometa 3,855.65, changarawe kutoka kilometa 29,116.57 hadi kilomita 102,358.14 na madaraja toka 2,812 hadi 6,620,”
“Fedha zitakazotumika kwenye mpango huu zinakadiriwa kuwa Shilingi trilioni 2.974,” amesema Ummy.
Ummy ameiagiza Tarura kufuata vigezo stahiki katika utekelezaji mpango huo, ikiwemo kuzingatia usawa katika ugawaji wa rasilimali fedha za ujenzi wa miundombinu hiyo.
“Aidha, fursa za kiuchumi na kijamii zipewe umuhimu, ili kuweza kuongeza mtandao wa barabara katika maeneo ya vijijini,” amesema Ummy.
Leave a comment