WANAWAKE vijana walioko kwenye taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania, wametakiwa kumiliki na kutumia vyema mitandao ya kijamii kwa ajili ya kudai haki za kijamii, kisiasa na kiuchumi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha … (endelea).
Hayo yamesemwa jana jijini Arusha, wakati wa uzinduzi wa mradi wa kuwajengea uelewa na ujasiri, wanawake vijana walioko kwenye taasisi hizo za elimu ya juu.
Mradi huo unashirikisha mashirika matatu ya kiraia ambayo ni Shirika la Wanahabari la Utetezi wa Jamii za Pembezoni (MAIPAC), Taasisi ya Uraia na Msaada wa Kisheria (CILAO) na Shirika la Kusaidia Ustawi wa Wanawake na Watoto (WOCWELS).
Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika jana Jumamosi, tarehe 20 Novemba 2021, Mkurugenzi wa CILAO, Odero Charles alisema vyuo vikuu vinavyohusika; ni Tumaini Makumira, Mtakatifu Agostino Centa ya Arusha na Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru-TICD)
Amesema lengo la mradi huo ni kuwajengea uelewa na ujasiri wanawake vijana walioko vyuoni kuweza kumiliki na kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kudai zao pasina woga wala vitisho.
“Tunawataka wanawake vijana waliopo elimu ya juu kutumia vyema mitandao kwa kupaza sauti dhidi ya ukatili wanaofanyiwa vyuoni,” alisema Charles.
Naye Mkurugenzi wa MAIPAC, Mussa Juma amesema katika mradi huo, kutakuwa na kampeni katika vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Amesema pia kutakuwa na mafunzo kuhusu usalama na ulinzi kwenye mitandao ya kijamii na kuhakiki usahihi wa taarifa .
“Wasichana mliopo kwenye taasisi za elimu ya juu, msiwe wanyonge katika kumiliki na kutumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kudai haki za kijamii, kisiasa na kiuchumi” amesema Juma
Kwa upande wake, Mary Mushi ambaye ni Mkurugenzi wa WOCWELS, amesema katika mradi huo kutakuwa na mafunzo kuhusu sheria na sera zinazolinda matumizi ya mitandao nchini
“Kutakuwa na midahalo kuhusu matumizi ya dijitali na fursa hivyo tunataka wasichana kwenye taasisi za elimu ya juu kutumia mitandao vizuri na tutatumia hashtags, maisha salama, fursa zaidi na digitali,” amesema
Wakizungumza katika uzinduzi huo, viongozi wa serikali za wanafunzi vyuo vya St Agustine, Makumira na taasisi ya maendeleo ya jamii Tengeru walieleza watashiriki vyema mradi huo kwani unamanufaa kwao.
Awatif Mshana, waziri wa Afya wa SAUT-Arusha amesema wanachuo wasichana wamekuwa waoga katika kutumia mitandao kutokana na baadhi ya watu kuitumia kuwadhalilisha.
“Tunaamini elimu hii itakwenda kutuunganisha wanachuo wasichana na kutumia vizuri mitandao,” amesema
Ester Koka wa Tumaini Makumira amesema wanasichana wengi chuoni wamekuwa hawatumii vizuri mitandao lakini yeye anatumia vizuri na amenufaika kupata fursa mbalimbali.
Joyce Athanas kutoka chuo Cha Maendeleo ya jamii Tengeru alisema anaimani kupitia mradi huu atakwenda kutumia mitandao vizuri na kupaza sauti juu ya ukatili vyuoni.
Ruth Usanga, mwanafunzi wa SAUT Arusha amewasilisha wanachuo wenye ulemavu alisema wengi wao wapo vijijini hawajui fursa zilizopo kwenye mitandao hivyo atakuwa balozi mzuri kumfikisha elimu vijijini.
Leave a comment