WATU zaidi ya 130 wameripotiwa kufariki dunia nchini Canada, baada ya kuathiriwa na joto kali lililoikumba nchi hiyo tangu Jumatatu ya tarehe 28 Juni 2021. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Kwa mujibu wa mitandao hiyo, watu hao walifariki dunia kati ya Jumatatu hadi leo Jumatano tarehe 30 Juni 2021, ambapo wazee wanaongoza katika idadi ya vifo hivyo.
Jeshi la Polisi nchini Canada, limesema idadi kubwa ya vifo ilitokea katika Mji wa Vancouver uliopo Wilaya ya Burnaby, ambapo watu 69 wamefariki dunia.
Mamlaka nchini Canada zinasema, kiwango hicho cha juu cha joto hakijawahi kushuhudiwa nchini humo, ambapo katika siku tatu mfululizo kiwango hicho kilikuwa nyuzi joto 49.9.
Maeneo yanayotajwa kuathirika na joto hilo ni Lytton, British Columbia, Alberta, Saskatchewan na Yukon.
Inadaiwa kuwa, Canada iliwahi kukabiliwa na changamoto hiyo miaka kadhaa iliyopita, lakini kiwango cha juu cha joto kilikuwa nyuzi 45.
Kufuatia changamoto hiyo, wananchi nchini Canada wametakiwa kuchukua tahadhari za kujikinga na athari za joto kali, huku wazee wakipewa kipaumbele katika uangalizi huo.
Leave a comment