RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameridhia uamuzi wa Serikali ya Indonesia wa kufufua shughuli za Kituo cha Mafunzo ya Kilimo kwa Wakulima Vijijini (FARTC) kilichopo Mkindo mkoani Morogoro. Anarippoti Maryam Mudhihir…(endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Agosti 2023 akiwa na mgeni wake, Rais wa Jamhuri ya Indonesia, Joko Widodo ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku mbili wakati wakizungumza na vyombo vya habari Ikulu Jijini Dar es Salaam.
Aidha, Rais Samia ameeleza kuwa kituo hicho kilianzishwa mwaka 1996 na serikali ya Indonesia ambayo ilichangia kwa kiasi kikubwa katika elimu ya kilimo kwa wakulima na kutoa mafunzo kwa wataalamu wa kilimo.
Pia amesema Tanzania na Indonesia zimekubaliana kuongeza biashara na uwekezaji kwa kuimarisha ushirikiano kati ya sekta za umma na binafsi katika maeneo ya viwanda, kilimo, nishati, madini, mafuta, gesi, uvuvi na utalii.
Vile vile, Rais Samia ameelezea kuwa mazungumzo yao yamebainisha nia ya Tanzania kupata uzoefu katika uzalishaji wa mafuta kutoka kwa Indonesia ambayo ni moja ya wazalishaji wakubwa zaidi wa mafuta ya mawese duniani.
Aidha, Rais Samia amesisitiza kuwa Tanzania imejidhatiti kuongeza uzalishaji wa mafuta ya kula ili kuacha kutegemea uagizaji wa mafuta kutoka nje ya nchi na hivyo kuokoa fedha za kigeni.
Nchi hizi mbili pia zimetiliana saini hati saba za makubaliano, ikiwemo sekta ya kilimo, nishati, ulizi, uvuvi na uchumu wa bluu, madini, pamoja na misamaha ya viza kwa wamiliki wa hati za kusafiria za kidiplomasia na huduma.
Leave a comment