INSPEKTA Jenerali wa Polisi nchini Tanzania, IGP Simon Sirro, amefanya mabadiliko madogo ya Makamanda wa Polisi, ikiwemo kumhamisha aliyekuwa Kamanda wa Jeshi la Polisi Mwanza, Muliro Jumanne, kwenda Kanda Maalum ya Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Jeshi la Polisi, Kamanda Muliro anachukua nafasi ya Kamishna wa Polisi, Camillius Wambura, aliyeteuliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, kuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya jinai (DCI), jana tarehe 30 Mei 2021.
Katika mabadiliko hayo, IGP Sirro amemhamisha Kamishna Msaidizi wa Polisi, Zuberi Chembera, kutoka Makao Makuu ya Upelelezi Dodoma, kwenda Makao Makuu ya Polisi Zanzibar, kuwa Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa jinai Zanzibar.
Kamanda Chembera anakuchukua nafasi ya Kamishna wa Polisi, Hamad Khamis Hamad.
Vilevile, Kamishna Msaidizi wa Polisi Stella Richard, amehamishwa kutoka kuwa Kamanda wa Kikosi cha Polisi Tazara, kwenda kuwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida.
Mabadiliko mengine yaliyofanywa na IGP Sirro, ni kumhamisha aliyekuwa Boharia Mkuu, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Ramadhan Ngh’anzi, kwenda kuwa Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza.
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Mwamini Rwantale, amehamishwa kutoka Kanda Maalum ya Dar es Salaam ambako alikuwa Mkuu wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimali watu, kwenda kuwa Kamanda wa Polisi Kikosi cha Tazara.
IGP Sirro amemhamisha aliyekuwaKaimu Kamishna wa Fedha na Logistiki Makao Makuu ya Polisi Dodoma, Naibu Kamishna wa Polisi, Lucas Mkondya, kwenda kuwa Mkuu wa Usalama Barabarani nchini.
Pia, IGP Sirro amemhamisha aliyekuwa Kamanda wa polisi wa mkoa wa Kipolisi Rufiji, Onesmo Lyanga, kwenda kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, akichukua nafasi ya Kamanda Gilles Muroto, ambaye anastaafu.
Leave a comment