MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (Duwasa), iko mbioni kufanya upanuzi wa mifumo ya majitaki, ili kukidhi kasi ya ukuaji wa jiji hilo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 31 Mei 2021 na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Duwasa, Mhandisi Aron Joseph, akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.
Mhandisi Joseph amesema, Duwasa inatarajia kutumia Sh. 161 bilioni, kwa ajili ya utekelezaji suala hilo, ikiwemo kujenga mabwawa 16 ya kutibu maji.
“Tuna mradi wa kujenga mabwawa ya kutibu maji 16, kwa sasa tuna mabwawa manne, ambayo yamezidiwa uwezo. Hivyo tunaenda kujenga mabwawa hayo kwenye eneo la Nzuguni B na tayari tumeshalipa fidia ya eneo hilo lenye ukubwa wa hekari 60, lililogharimu zaidi ya Milioni 600 kulipata,” amesema Mhandisi Joseph.
Mhandisi Joseph amesema, fedha hizo ni mkopo wa gharama nafuu kutoka Serikali ya Korea.
“Gharama za utekelezaji wa mradi huo ni kiasi cha Sh. 161 bilioni, sawa na Dola za Marekani 70 Milioni ambazo ni mkopo wa gharama nafuu kutoka serikali ya Korea.
Mradi huu upo katika hatua nzuri na tumeshirikiana na Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Fedha, kuhakikisha mahitaji yote muhimu yanapatikana,” amesema Mhandisi Joseph.
Leave a comment