IDADI ya vyombo vya habari nchini Tanzania imeendelea kuongeza mwaka hadi mwaka ambapo kwa mwaka 2021/22 idadi hiyo imeongezeka kwa kasi. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Habari na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye leo Ijumaa tarehe 20 Mei 2022 akiwasilisha bajeti ya wizara kwa mwaka 2022/23.
Nape amesema vituo vya kurusha matangazo ya redio vimeongezeka kutoka vituo 200 mwaka 2021 hadi kufikia vituo 210 Mwezi Aprili, 2022 sawa na ongezeko la asilimia 5 huku vituo vya televisheni vimeongezeka kutoka vituo 50 na kufikia vituo 56 sawa na ongezeko la asilimia 12.
Ameongeza Cable Television zimeongezeka kutoka 40 hadi 59 sawa na ongezeko la asilimia 47.5 na magazeti yameongezeka kutoka 272 na kufikia 284 sawa na ongezeko la asilimia 4.4.
“Serikali imeendelea kuweka mazingira rafiki ya matumizi ya teknolojia za Utangazaji hasa maudhui mtandaoni ambayo pia yamechangia kuongeza ajira kwa vijana,” amesema Nape.
Amesema kufikia Mwezi Aprili, 2022 televisheni mtandao zimeongezeka kutoka 552 hadi 663 sawa na ongezeko la asilimia 20.1, blogu zimeongezeka kutoka 134 hadi 148 sawa na ongezeko la asilimia 10.4 na redio mtandao zimeongezeka kutoka 25 hadi 27 sawa na ngezeko la asilimia 8.0.
Leave a comment