MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga kutolea uamuzi juu hatma ya dhamana ya aliyekuwa Rais wa klabu ya Simba, Evance Aveva na Makamu wake, Godfrey Nyange (Kaburu) baada ya upande wa Serikali kuiarifu mahakama hiyo nia ya kukata rufaa kupinga uamuzi wa kufutiwa kwa makosa ya utakatishaji fedha. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Tarehe 19 Septemba, 2019, Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba aliamua kufuta mashtaka yote ya utakatishaji fedha kwa watuhumiwa hao ambapo siku ya pili yake Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DPP) kupitia Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon aliijuza mahakama hiyo kuwa (DPP) anania ya kukata rufaa.
Mshtakiwa mwengine kwenye kesi hiyo ni Zakharia Hanspope ambaye hajashtakiwa kwenye makosa ya utakatishaji fedha.
Leo Tarehe 23 Upande wa Serikali imewasilisha hoja juu ya kwanini wanapinga uamuzi huo ambapo Wakili Wankyo amedai mahakamani hapo kuwa kwa mujibu wa sheria DPP akitoa taarifa ya kusudio la kukata rufaa Mahakama kuu rufaa inakuwa tayari.
Ameiomba mahakama hiyo kusimamisha dhamana za washtakiwa hao mpaka rufaa hiyo itakaposikilizwa kwa kuwa zinatokana na kufutwa kwa mashtaka ya utakatishaji fedha ambapo upande huo umeeleza kufutwa kwa makosa hayo ndiyo kumelekea kupatikana kwa dhamana.
Baada ya hoja hizo Wakili wa Utetezi, Nehemia Nkoko amedai mahakamani hapo Upande wa Mashtaka haujapinga dhamana ya washtakiwa hao na kwa kuwa mahakama hiyo ilishatoa dhamana kwa watuhumiwa hao haoni sababu ya kuzuiliwa.
Hakimu Simba ameahilisha shauri mpaka tarehe 27 Septemba mwaka huu kwa ajili ya kutoa uamuzi juu rufaa hiyo.
Leave a comment