OMBI la kusafiri nje ya nchi la Dk. Vincent Mashinji, Katibu Mkuu Chadema na Ester Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini, limekataliwa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam imekata ombi hilo kwenye kesi ya uchochezi 211/2018 inayowakabili wanasiasa hao.
Leo tarehe 25 Septemba 2019, Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba ameeleza, kwa kuwa watuhumiwa ni wabunge, iwapo ataruhusu hivyo, kesi hiyo haitaisha.
Katika kesi hiyo, washitakiwa wengine ni Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema-Taifa, John Mnyika, Naibu Katibu Bara na Salum Mwalimu, Naibu Katibu Zanzibar.
Wengine ni Halima Mdee, Mbunge wa Kawe; Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini; Mchungaji Peter Msigwa, Mbunge wa Iringa Mjini na John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini.
Kutokana na maombi ya ruhusu ya Matiko na Dk. Mashinji, yaliyowasilishwa jana tarehe 24 Septemba 2019 mahakamani hapo na wakili muungoza jopo la utetezi Prof. Abdallah Safari, Hakimu Simba ameona hakuna sababu ya kutoa ruhusa hiyo.
Prof. Safari aliieleza mahakama kuwa tarehe 26 Septemba – 6 Oktoba 2019, Dk. Mashinji atakuwa safarini Uengereza katika majukumu ya chama. Na kwamba, wanapaswa kuwaandaa mashahidi waliojeruhiwa kwa risasi ili kuwaleta mahakamani hapo.
Prof. Safari amedai mahakamani hapo, mshitakiwa wa tano (Matiko), amealikwa kupitia Ofisi ya Bunge kuanzia tarehe 25 – 28 Septemba mwaka huu kwenda Kigali, Rwanda.
Pia ameeleza, tarehe 13 Septemba -18 Oktoba 2019, Matiko amealikwa kwenye Bunge la Umoja wa Ulaya kama Mjumbe wa Afrika.
Katika uamuzi wake Hakimu Simba amesema, kesi ipo kwenye hatua ya utetezi na kwamba akikosekana mtuhumiwa mmoja, kesi itakwama.
Amesema, kesi hiyo inalalamikiwa kuchelewa “ukizingatia hoja za Wakili Profesa kuwa wanamashahidi wengi …”
Hakimu Simba ameaharisha shauri hilo mpaka tarehe 7, 8, 9, 10 na 11 ambapo itasikilizwa kwa siku tano mfululizo.
Leave a comment